Msimu mpya wa Ligi Kuu Kenya kwa mwaka 2018/19, umeanza kutimua vumbi nchini humo huku beki wa Kitanzania, Aman Kyata anayeichezea Nakumatti FC akiweka rekodi.
Kyata na Nakumatti yake ambayo kwa sasa inatambulika kama Mount Kenya United, aliweka rekodi ya kuwa Mtanzania wa kwanza kufunga bao msimu huu, licha ya timu yake kuwa na mwanzo mbaya kwenye Ligi.
Desemba 9, Kyata alifunga bao hilo kwenye mchezo dhidi ya Sofapaka ambao ulimalizika kwa Mount Kenya United kufungwa kwa mabao 2-1.
Sio Kyata pekee ambaye ni Mtanzania anayecheza Ligi Kuu Kenya, wapo wengine kama vile; Abdallah Hamis wa Bandari, Jamal Mwambeleko na Peter Manyika JR wanaochezea KCB na Marcel Kaheza wa AFC Leopards.
Baadhi ya nyota hao wa Tanzania wamezungumza na Spoti Mikiki na kueleza namna walivyouanza msimu mpya wa KPL na kueleza malengo yao.
Unaweza kusema ni kama Hamis hakuwa na bahati ya kuuanza msimu vizuri kutokana na kusumbuliwa kwake na majeraha ya ugoko hivyo aliukosa mchezo dhidi ya Gor Mahia.
Hamis anasema anajivunia ubora wa kikosi chake ambacho pamoja na kukosekana kwake waliweza kupata matokeo ya ushindi mbele ya mabingwa hao watetezi wa KPL.
“Nimerejea kwa sasa na mchezo niliokosa ni ule wa ufunguzi, tunaamini kuwa huu ni msimu wetu, tutapambana ili tufikie malengo ya kutwaa ubingwa wa Ligi.
“Msimu uliopita tuliteleza mwishoni ndio maana tulimaliza nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi kama maandalizi kujiandaa na huu msimu tumefanya makubwa kwa kuwa na michezo mingi ya kirafiki, “ anasema.
Beki wa kati wa Mount Kenya United, Aman Kyata anasema malengo yake pamoja na klabu yake ni kumaliza msimu kwenye nafasi za juu.
Kyata ambaye amekuwa akitumia nguvu na akili kwenye uchezaji wake, anasema hakuna kinachomfanya akose amani kama timu yake inapokuwa kwenye hatari ya kushuka daraja.
“Tumepoteza gemu mbili za mwanzoni mwa msimu, tunatakiwa kuzinduka na kuanza kupata matokeo ya ushindi ili tuanze mapema kutojiweka katika mazingira mabaya.
“Naamini tunatimu nzuri ya kukabiliana na yeyote atakayekuwa mbele yetu, kikubwa kila mmoja wetu anatakiwa kuongeza kiwango chake cha kujituma,” anasema.
Hali ni tete kwa timu ngeni ya KCB, Ligi Kuu Kenya yenye wachezaji wa Kitanzania, Jamal Mwambeleko ambaye ni beki wa kushoto na kipa Peter Manyika JR.
Mwambeleko aliyeanzia Mbao FC akatua Simba ambako alikuwa na msimu mbaya na kupelekwa Singida United.
Baada ya kutua Singida United, alikumbana na tatizo la kiuchumi. Timu iliyumba kiasi cha kushindwa kuwalipa wachezaji wake.
Baada ya hapo wakavunja mkataba na kuamua kutafuta timu Kenya na wote kwa pamoja wakatua KCB.
Amejiunga na AFC Leopards kwa mkopo wa miezi sita.
“Nimekuja hapa kwa ajili ya maisha ya soka, lakiini kama Simba watanihitaji nitarudi lakini vinginevyo nitaendelea na maisha yangu ya kutafuta.
“Nilikwenda Simba nilipanga iwe daraja, ndoto yangu ni kucheza nje ya Tanzania na AFC Leopards japo ni mkopo ni kama imefungua njia ya mimi kucheza soka nje.”