MASHABIKI wa Simba presha zimewapanda baada ya kusikia kocha wao kipenzi, Masoud Djuma yupo mbioni kutemwa na klabu hiyo, ikielezwa ishu ni nidhamu mbovu alivyonayo, lakini imebainika Kocha Mkuu, Patrick Aussems anahusika.
Ishu ya kocha huyo kutimuliwa Simba zilivuja usiku wa juzi Jumapili baada ya mabosi wa Bodi ya Ukurugenzi ya klabu hiyo kukutana na Mbelgiji kumjadili
Kocha Masoud ambaye amekuwa kipenzi cha mashabiki wa klabu hiyo.
Inaelezwa kuwa, Aussems amesisitiza kutomtaka Msaidizi wake huyo kwa madai ana nidhamu mbaya, huku baadhi ya nyota wa klabu hiyo pia wakimchongea Mrundi huyo kwamba ‘hajatulia’ kabisa.
“Ni kweli Masoud amejadiliwa na Kocha Mkuu amesisitiza hamtaki kwa vile nidhamu yake haimvutii, lakini pia jamaa anajiona bonge la kocha na anaongea sana kwa wanachama na mashabiki, jambo ambalo halina afya kwa timu.”
Kigogo mmoja wa Simba alisema, Masoud tangu aje ametengeneza himaya yake ndani ya klabu jambo lililomfanya hata Pierre Lechantre kumtakaa, lakini kiu yake
ya kutaka kuwa Kocha Mkuu ndiyo imewatibua zaidi.
“Unajua Masoud ana uwezo wa kufundisha, lakini kitu kibaya anajiona bonge la kocha na anatamani awe kocha mkuu jambo ambalo kwa sasa kuwa hivyo ndani ya Simba haiwezekani na bado sana,” alisema kigogo huyo (jina kapuni).
“Tutamuita pia katika kikao chetu kama tulivyofanya na Aussems na kumuliza kwa nini hana nidhamu kwa bosi wake hadi kufikia maamuzi ya kumkataa, najua naye
atajitetea kwa nafasi yake,” alisisitiza kigogo huyo.
“Masoud pia ana siasa mbaya kwani anafikia hatua ya kuongea na wanachama kutafuta nguvu kutoka kwao, jambo ambalo si zuri na hata uongozi hauridhishwi na jambo hilo lakini hata wachezaji wanasema hayupo kitaaluma zaidi.
“Pia KOcha Aussems ametuambia hata kama Masoud akiondoka uongozi Simba usiingie gharama ya kutafuta Kocha Msaidizi kwani jukumu hilo atalifanya Adel Zrane ambaye ni kocha wa viungo,” alisema kigogo huyo.
Kocha Masoud Djuma alipotafutwa na Mwanaspoti alisema anashangaa kuwepo kwa taarifa hizo, akidai kuwa sio mara ya kwanza kuzushiwa kuondoka Simba,
kwani alishafanyiwa hivyo akiwa Kenya katika mashindano ya Sport Pesa.
“Sifahamu hizi taarifa zinatoka wapi, sijakutana na mabosi wa Simba na hata wao hawajanifahamisha lolote na tangu kocha Aussems amefika tumekuwa tukifanya
kazi kwa ushirikiano mkubwa, sasa sijui haya yatokea wapi,” alisema Masoud.
Kocha huyo aliyejiunga na Simba akitokea Rayon Sports, alisema; “Nina imani kubwa ya kuendelea kuwepo Simba kwa kazi ninayofanya na hata kama imefika
wakati wa kuondoka, nataka niondoke salama bila uhasama.”
“Najua muda wa kuondoka ukifika hakuna wa kuuzuia kwani hata kuja kwangu kulitokana na mipango ya Mungu, lakini hivyo vinavyoelezwa sijui vinatokea wapi
na hii suio mara ya kwanza kuzushiwa ishu kama hizi, ila ngoja tuone,” alisema.
Kaimu Rais wa Simba, Salim Abdallah ‘Try Again’ alipoulizwa juu ya ishu nzima ya kumjadili na kufikia maamuzi ya kumtema Masoud kwa madai ya ukosefu wa nidhamu alisema kwa kifupi;
“Mambo ya Simba yanazungumzwa tu. Hata hayo ya Masoud ni hivyo, ila naomba nipigie simu saa tisa nitakuwa na majibu kamili,” alisema Try Again aliyechukua
nafasi ya Rais Evans Aveva ambaye na Makamu wake, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ wanakabiliwa na mashtaka ya utakatishaji fedha za klabu hiyo.
Hata hivyo baadaye alipopigwa simu yake ilikuwa ikiita bila kupokelewa.