Dar es Salaam. Kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera ameungana na Watanzania kuomboleza msiba wa Mkurugenzi wa Vipindi na Uzalishaji, wa Clouds Media, Ruge Mutahaba ambaye amefariki dunia jana Jumanne jioni nchini Afrika Kusini alikokuwa akitibiwa.
Zahera aliandika kwenye ukurasa wake wa Instagram akisema hajawahi kuonana na Ruge isipokuwa amekuwa akisoma baadhi ya kazi zake na kupata historia yake kupitia kwa marafiki.
Amesema tasnia ya habari na burudani imempoteza mtu wa muhimu jambo ambalo hata viongozi wanamlilia.
Zahera aliweka picha kwenye ukurasa wake iliyokuwa na nakuu ya Ruge enzi za uhai wake ikisema “ Msimamo wa kweli ni ule unaoweka leo bila kujali wala kuhofia juu ya lolote litakalotokea kesho.”