Dar es Salaam. Mtibwa Sugar inaondoka leo kwenda Uganda ikiwa na matumaini ya kufanya vyema katika mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya KCCA.
Mtibwa itacheza na KCCA baada ya kusonga mbele kwa ushindi wa jumla wa mabao 5-1 iliyopata dhidi ya Northern Dynamo ya Shelisheli.
Kocha wa Mtibwa, Zuberi Katwila alisema ametumia mikanda ya video ya KCCA ili kupata njia bora ya kupata ushindi katika mchezo huo wa Jumamosi wiki hii.
Katwila alisema video hizo zimewapa taswira ya kubaini kasoro za wapinzani wao, hivyo amejipanga kupata matokeo mazuri.
Kocha huyo alisema kuwa amefanyia kazi tatizo la kupoteza nafasi za kufunga mabao ambalo lilionekana katika mchezo dhidi ya Dynamo.