KOCHA msaidizi wa Azam, Vivier Bahati ambaye anakiongoza kikosi hicho kwenye Kagame Cup msimu huu amewamwagia sifa wachezaji wake kwa kiwango wanachokionyesha kwenye mashindano hayo.
Vivier ambaye ni raia wa Burundi ameeleza kuwa wachezaji wake wameweza kumuelewa haraka na kutengeneza muunganiko mzuri kwa muda mchache waliokaa pamoja.
"Ukiangalia kikosi hiki cha Kagame Cup tunatumia wachezaji kutoka timu tofauti tofauti. wapo waliokuwa timu za vijana na wengine walikuwa kwa mkopo hivyo hawajapata muda wa kuzoeana lakini wanajitahidi kucheza kwa pamoja.
Nawapongeza kwa hilo na kadri siku zinavyozidi kwenda naona wanazidi kuimarika na kutengeneza mshikamano ambao utatusaidia mbeleni," alisema Vivier.
Azam ambao ni mabingwa mara mbili wa michuano hiyo, msimu huu ipo kundi B, pamoja na timu za Messager Ngozi ya Burundi, KMKM ya Zanzibar, na KCCA ya Uganda na mechi ya kwanza ilishinda bao 2-0 dhidi ya KCCA mabao yote yakifungwa na Paul Peter na jana ikashinda 1-0 dhidi ya Messanger Ngozi ya Burundi na kufikisha alama sita kileleni mwa kundi hilo.