Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kauli ya kwanza ya Manara 2018 kuhusu majibu ya FIFA

1025 IMG 9228 2 TZW

Thu, 4 Jan 2018 Chanzo: bongo5.com

Baada ya kuuaga mwaka 2017 na kuingia mwaka mpya  afisa habari wa klabu ya Simba, Haji Manara ameelezea changamoto alizokabiliana nazo mwaka uliyopita ambapo ikiwemo na rufaa yao kwa shirikisho la soka duniani FIFA dhidi ya kupinga maamuzi ya TFF ya kupokwa pointi tatu.

Msemaji wa Simba SC

Awali ya yote tumshukuru sana Mungu mwenyezi kwa kutuwezesha sote kuumaliza mwaka 2017 na kuuingia mwaka huu mpya wa 2018.

Mwaka tulioumaliza ulikuwa na changamoto nyingi sana kama ilivyo kwa miaka yote ya nyuma.

Changamoto tulizopitia ni za kawaida sana ingawa nyingine zilikuwa ngumu sana, kiasi cha kwamba zimeacha doa kwenye maisha yetu.

Mojawapo ya changamoto iliyonigusa sana mwaka jana, ni kushtakiwa kwa viongozi wakuu wa klabu nnayoisemea ya Simba.

Kufunguliwa kwa Shauri lile sio tu kulinihuzunisha, bali kulinifanya niwe muoga sana kwa kila kitu, ila kama nilivyoandika ni changamoto tu na mwanadamu huna budi kupitia mitihani ya aina hii ili kukamilisha ubinadamu wako, sote tumuombe Mungu aiwezeshe kesi hii iishe haraka na haki ipatikane kwa pande zote.

Mwaka jana pia kama klabu na kama Timu tulipata changamoto kubwa ya vyombo vyenye maamuzi ya kuongoza Soka nchini, kutoitendea haki klabu yetu kwa mambo kadha wa kadha, sio nia yangu kufukua makaburi, lakini lazma tujikumbushe ile kadhia tata ya kadi tatu za njano, ambayo kwa maksudi kabisa waliokuwa viongozi wa TFF waliamua kulipindisha jambo lile ili tu waliepanga awe bingwa kupata walichopanga.

Haiwezekani na ntaendelea kuamini kamati iliyofanya maamuzi ya kuipoka Simba points tatu, haikuwa na mamlaka yoyote ya kutolea maamuzi ya jambo liliotokea uwanjani, Sote tunajua kila shauri hutolewa uamuzi na chombo ‘Makhsuus’.

Itakuwa ajabu ya karne eti Mahakama ya Ardhi kutolea maamuzi kesi za ubakaji, au kamati ya Bunge ya maadili kutolea uamuzi kesi za Trafik, ni kituko kikubwa kuwahi kutokea nchini…. kwangu ulikuwa uonevu mkubwa zaidi kuwahi kutokea nchini, Lakini yalishaisha na sisi kama klabu tuliamua kusonga mbele zaidi.

Ni kweli Simba iliamua kulalamika FIFA baada ya kuona hatutapata haki kwa TFF ile, lakini chombo hicho kikubwa zaid duniani kilitujibu kwa njia ya DHL,ya kwamba tutumie vyombo vya ndani kwenye Shirikisho na ushauri wao kwetu pia ulilenga kuzingatia muda wa malalamiko yetu.

Busara ya uongozi wa Simba chini ya kaimu Rais wa Simba Salum Abdallah kwenye jambo hili ilikuwa kubwa sana, kwa kuwa majibu ya FIFA yalichelewa na teyari uongozi mpya wa TFF ulishaingia madarakani, na kwa kuwa hata waliobebwa wanajua kuwa walibebwa na kwa kuwa hatukutaka kuwapa msuguano na wadau wake TFF mpya, ukizingatia walifungua ukurasa mpya kwenye Soka nchini, Simba iliamua kuachana na rufaa ili ijikite kwenye msimu huu tulionao sasa.

Ifahamike pia kombe la Ubingwa wa msimu uliopita lilikabidhiwa haraka haraka ili kutoa ugumu kwa haki sio kutendeka bali kuonekana imetendeka.

Nyote mnafahamu kitendo cha dhulma ile ilinipelekea mimi kufungiwa mwaka mmoja na faini ya Shilingi milioni tisa, Lakini nishukuru kamati ya Nidhamu ya TFF na uongozi wa Shirikisho kwa kuniondolea adhabu ile iliyotolewa bila kunipa haki ya kusikilizwa (Natural justice).

Kwa kweli kipimo cha uonevu msimu uliopita kinahitaji kiwekwe kwenye maandishi ya ‘Riwaya’ itakayosomwa na vizazi vingi vijavyo..Ila kwa kadri nijuavyo uongozi wa klabu, mm mwenyewe na wanasimba wote wamesamehe, tusonge mbele, yaliyopita c ndwele tugange yajayo.

Mwaka jana klabuni pia tulianza mchakato mkubwa wa kuingia kwenye mabadiliko ya kimuundo na kimfumo ya klabu yetu. Mchakato huu ulienda vzuri sana na tupo kwenye hatua za mwisho mwisho kuwezesha klabu kuanza rasmi kuutumia muundo huo wa hisa.

Muundo huu utaiwezezha klabu yetu kuwa klabu tajiri miongoni mwa vilabu tajiri Africa, Utajiri huu tunaamini utaiwezesha klabu kuwa na uwezo mkubwa wa kujiendesha na kuwa rasimali zitakazotuwezesha kuwa na mafanikio ya ndani na nje ya Uwanja.

Kwenye mchakato huu pia tulipata changamoto mbalimbali. lakini Alhamdulillah kwa sehemu kubwa tumevuka salama. na kwa sasa milango ipo wazi kwa wale waliotaka kukwamisha kujirudi na sote kwa pamoja tuje tujenge Klabu yetu..ukizingatia tuna kauli mbiu isemayo SIMBA NGUVU MOJA

Kwenye changamoto hakukosi mafanikio. licha ya kukoseshwa ubingwa kwa figisu figisu.Simba ilifanikiwa kushinda kikombe cha Shirikisho ambacho kimetuwezesha kupata nafasi ya kuwakilisha nchi mwaka huu kwenye michuano inayoandaliwa na Shirikisho la Soka barani Afrika(Caf).

Msimu huu uongozi wenu umejitahidi kuwasajili wachezaji bora zaid ambao sio tu waturejeshee ubingwa wa ligi, bali kufanya vema kwenye michuano hyo ya Afrika.

Kwa sasa bado tunaongoza ligi kuu na wachezaji wetu hawadai shilingi ya mishahara, na wanajua kiu ya wanasimba msimu huu.. pia uongozi unatambua changamoto tuliyokutana nayo msimu uliopita, wale wanaodhani msimu huu kutakuwa na yale yale ya msimu uliopita tuwaambie wasubiri, Sababu hatuamini TFF hii inae bingwa iliempanga na hakutakuwa na uchakachuaji wa ratiba na waamuzi. basi InshaAllah bingwa halali atapatikana msimu huu.. na kwa maandalizi tuliyoyafanya na kwa matakwa ya Mungu Simba itachukua ubingwa safari hii.. hilo ndio lengo letu na dhamira ya klabu. kubwa tunawaomba wanasimba tudumishe umoja na mshikamano wetu. tuvumiliane, tukosoane kistaraabu, tusitoe fursa kwa wapinzani wetu na kwa wachezaji watambue kile alichokisema Bwana MO pale Ukumbi wa Mwalimu Nyerere.. thamani ya kuvaa jezi ya Simba, thamani ya kuichezea Simba, sote tutambue sisi ndio klabu kubwa nchini, klabu ya watu, klabu maarufu zaid ndani na nje ya nchi na tujue nini tunataka msimu huu na mwaka huu kwa ujumla.

Mwisho niwaombe sote tuendelee kuwaombea viongozi wetu wa nchi. Wale wa Serikali wakiongozwa na Rais wetu Mh John Magufuli, wale wa vyama vya siasa, na wale wa taasisi zingine, hekima,busara,kumjua Mungu,upendo na uzalendo na kwa viongozi wa TFF tuwaombee waendelee kutenda haki.

Asionewe mtu wala asipendelewe mtu. klabu zote ziwe sawa.

Ratiba iwe rafiki kwa klabu zote.

Waamuzi wachezeshe kwa haki mechi zote, tunajua mapungufu ya kibinadaam yapo ila mapungufu hayo yasiwe yanawapa upendeleo timu moja tu.

Sote tukiamua tunaweza kwa maslah mapana ya mchezo wa Soka nchini.

Kwa niaba ya Uongozi mzima wa klabu. benchi la ufundi. wachezaji, wanachama, washabiki wote wa Simba niwaambie

Happy New year 2018

IMETOLEWA NA….

HAJI S MANARA

Mkui wa Habari Simba Sc

SIMBA NGUVU MOJA

Chanzo: bongo5.com