MECHI ya watani wa jadi Simba dhidi ya Yanga imepangwa upya kuchezwa Julai 3 ikiwa ni mchezo wa raundi ya pili katika msimu huu.
Timu hizo katika raundi ya kwanza zilitoka sare 1-1 na katika mchezo wa raundi ya pili uliotakiwa kuchezwa Mei 8, mchezo haukufanyika baada ya kutokea sintofahamu katika timu hizo mbili.
Baada ya mchezo huo kuhairishwa Serikali iliingia kati kutokana na vuta nikuvute, kisha waliziagiza mamlaka husika (TFF na TPLB) kutoa upya tarehe ya mchezo huo kurudiwa.
Ratiba iliyotolewa leo na Bodi ya Ligi imeonyesha mchezo huo utachezwa saa 11:00 jioni katika uwanja wa Benjamin Mkapa.
Wakati mchezo huo ukipangiwa tarehe, viporo viwili kayi ya Simba na Namungo navyo vimepangiwa rasmi tarehe yq kucheza baada ya kutocheza mechi yoyote msimu huu.
Namungo wataanza kuikaribisha Simba Mei 29 katika uwanja wa Majaliwa kisha marudiano utachezwa Julai 18 katika uwanja wa Benjamin Mkapa.
Kiporo cha Namungo dhidi ya Gwambina, mchezo huo utachezwa Mei 26 katika uwanja wa Majaliwa, Ruangwa.