England. Timu ya Manchester City imekoleza mbio za ubingwa Ligi Kuu England baada ya kuifunga Leicester City bao 1-0 kwenye mchezo uliopigwa jana Jumatatu usiku.
Bao pekee la Manchester City liliwekwa wavuni na Vincent Kampany dakika ya 70 kipindi cha pili na kuifanya timu hiyo kufikisha alama 95 kileleni huku Liverpool wakiwafuatia nafasi ya pili wakiwa wamejikusanyia alama 94.
Kocha wa Manchester City, Pep Guardiola amesema ushindi huo umempa furaha na kusisitiza kuwa bado wanahitaji ushindi kwenye mechi inayofuata ili kutawazwa kuwa mabingwa wa msimu huu.
Alisema anajipanga kwa mchezo unaofuata wikiendi inayokuja dhidi ya Brighton ambao utawapa tiketi ya ubingwa wa England msimu huu.
Nyota wa mchezo huo, Kampany alisema timu yake imecheza na timu nzuri ambayo ipo kwenye nafasi sita za juu Ligi Kuu England.
Hata hivyo alisema msimu uliopita haukuwa mzuri kwakwe kutokana na kushindwa kufunga mabao ya kutosha lakini kipindi hiki amefunga katika wakati mwafaka.
Alisema kwenye mchezo huo alicheza kama ndio mechi yake ya mwisho huku akiwa ameweka akilini kwamba kila mchezo wanaoingia uwanjani kwa sasa ni muhimu kwao.
Nyota hao wa Manchester City; David Silva, Vincent Kampany na Gabriel Jesus walijikuta wakilimwa kadi za njano kwenye mchezo huo.