Dar es Salaam. Mshambuliaji wa Simba, Meddie Kagere anaamini msimu ujao wa Ligi Kuu Bara anaweza kuvunja rekodi ya mwaka 1999 iliyowekwa na nyota wa zamani wa Yanga, Mohammed Hussein ‘Mmachinga’.
Mmachinga anashikilia rekodi ya kuwa mshambuliaji ambaye amewahi kufunga mabao mengi zaidi ndani ya msimu mmoja akiwa kwenye kiwango bora, mwaka 1999 aliifungia Yanga mabao 26.
Kagere ambaye msimu uliopita alipachika mabao 23, alisema hakuna kinachoshindikana kikubwa ni kuendelea kushirikiana na wachezaji wenzake.
Mshambuliaji huyo alisema idadi ya mabao aliyofunga msimu uliopita siyo kwa uwezo na akili zake pekee, bali pia ushirikiano kutoka kwa wenzake ambao alikuwa akicheza nao kwenye kikosi cha Simba.
“Kila siku zimekuwa zikiwekwa rekodi na nyingine zikivunjwa, kwa hiyo suala la kuvunja hiyo rekodi ni jambo ambalo linawezekana, nilikuwa kwenye nafasi ya kuifikia rekodi hiyo, lakini siyo mbaya hata kwa idadi ya mabao niliyofunga,” alisema Kagere.
“Najiona kuwa na mawazo ya kutaka kufunga zaidi msimu ujao kwa lengo pia la kutaka kuisaidia timu yangu kuendelea kufanya vizuri kuanzia kwenye ligi hadi katika mashindano ya kimataifa.”
Pia Soma
- Azam yaifuata Simba
- Teknolojia yaibua utata mabingwa Afrika
- Sarri mguu ndani, nje Chelsea
- Ronaldo awataja watano, amtosa Cristiano