Baadhi ya vifaa hivyo ni jezi, mipira, soksi, viatu, ambavyo vimetolewa na Kampuni ya Silent Ocean na kukabidhiwa kwa Kamanda ya Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, ACP Ramadhan Kingai.
Akipokea msaada huo kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Simon Sirro, Kamanda Kingai, alisema mashindano hayo yatashirikisha Jeshi la Wananchi, Polisi, JKT, Magereza, Zimamoto na vikosi vya kanda kutoka Zanzibar.
Sirro alishukuru kupata msaada huo wa vifaa vya michezo kwa sababu utaondoa unyonge wa kutokuwa navyo na utaongeza ari ya mazoezi kwa wanamichezo wa vikosi vyote wanaoendelea na mazoezi.
Mkuu wa Michezo wa Jeshi la Polisi, ACP Jonas Mahanga, alisema mashindano hayo yanalenga kukuza uhusiano katika vyombo vya ulinzi na usalama nchini na yamekuwa yakifanyika kila mwaka.
"Mwaka jana hatukufanya kutokana na ugonjwa wa corona, lakini sasa hali imetulia ndio maana wanamichezo wetu wako kambini wakiendelea kujifua kwa ajili ya kushiriki mashindano hayo," alisema ACP Mahanga.
Mwakilishi wa Silent Ocean, Mohamed Kamilagwa, alisema majeshi mengi yalikuwa yameomba vifaa vya michezo, lakini muda ukawa mchache wakaamua kuanza na Jeshi la Polisi.