Mtanzania, Gabriel Geay ameshika nafasi ya pili kwenye mashindano ya mbio ndefu (42km), Valencia Marathon, akitumia saa 2:03:00, nyuma ya Kelvin Kiptum wa Kenya aliyeshinda akitumia saa 2:01:53.
Geay amekuwa mwanariadha wa kwanza nchini kufuzu kushiriki mashindano ya dunia mwakani yataanza Agosti 19-27 huko Budapest, Hungary.
Kocha wa mwanariadha huyo, Thomas Tlanka alisema kama atakimbia muda mzuri basi atafuzu kuowakilisha nchi kwenye Olimpiki 2024 huko Paris Ufaransa.
Alisema muda wa saa 2:03:00 aliotumia kumaliza mbio ya Valencia Marathon jana umempa tiketi ya kufuzu kuchuana kwenye mashindano ya dunia.
Geay alimaliza wa pili na kutwaa medali ya fedha jana kwenye mbio hiyo, muda ambao pia umevunja rekodi ya taifa ya marathoni aliyokuwa akiishikiria ya saa 2:04:55.
“Ni muda mzuri kwake na kwa taifa, ambao kama atakimbia muda huo au chini ya hapi kwenye mashindano ya dunia mwakani, hakuna shaka atafuzu kuiwakilisha nchi kwenye Olimpiki,” alisema Tlanka.
Mkenya, Kelvin Kiptum aliibuka kinara akitumia saa 2:01:53 akimpiku Geay kwa dakika 01:07 wakati ‘ndugu’ yake, Alexander Mutiso akihitimisha tatu bora akitumia saa 2:03:29.
Nyota mwingine wa dunia wa masafa marefu raia wa Ethiopia, Tamirat Tola alimaliza wa nne akitumia saa 2: 03: 40 kumaliza mbio hiyo jana.