Inaripotiwa kuwa klabu ya FC Barcelona ya Hispania ipo tayari kumuuza kiungo wao Frankie de Jong kwa ada ya uhamisho ya pauni million 75 ambayo ni zaidi ya billioni 232 kwa pesa za kitanzania. Manchester City inatajwa kuwa timu ya kwanza iliyoonyesha nia ya kumsajili.
Barcelona ipo kwenye harakati za kujijenga upya chini ya kocha mpya Xavi Hernandez, na wanahitaji kuboresha kikosi kwa kusajili wachezaji wapya na kwa sasa hawapo vizuri kiuchumi hivyo wanahitaji kuuza baadhi ya wachezaji ili kuongeza mapato ya klabu.
De Jong anaonekana kuwa mchezaji wa kwanza kuuzwa ili klabu ipate pesa na thamani yake inatajwa kuwa ni Pauni million 75 ambayo ni zaidi ya billion 232 za kitanzania. Kiungo huyo wa kimataifa wa Uholanzi mwenye umri wa miaka 24 alijiunga na FC Barcelona mwaka 2019 akitokea Ajax na ilionekana FC Barcelona mpya itatengenezwa kumzunguka yeye, na alikuwa moja kati ya wachezaji muhimu wa timu hiyo chini ya kocha Ronald Koeman.
Ripoti zinadai Manchester City ni moja ya timu inayopigiwa upatu kumsajili mchezaji huyo, na inaripotiwa kocha wa Man City Pep Guardiola anatafuta kiungo atakaeiwezesha timu kuwa na umiliki mkubwa wa mpira na mwezi uliopita iliripotiwa Manchester City na Barcelona walikuwa tayari kubadilisha wachezaji, ambapo Manchester City walikuwa tayari kumtoa Raheem Sterling na Barcelona Frankie de Jong.
Msimu huu ni wa 3 kwa De Jong akiwa na wakali hao kutoka Catalunya ameshaichezea michezo 106 amefunga mabao 9 na ameshinda kombe moja la Copa del Rey msimu wa 2020-21.