Dereva wa magari ya Rally Asad Khan (50) kutokea Kenya amefariki dunia jana katika hospitali ya Avenue alikokuwa akipatiwa matibabu.
Taarifa kutoka Kenya zinaeleza kuwa Asad alijeruhiwa vibaya baada ya kushambuliwa na mpenzi wake Maxine Wahome ambaye pia ni dereva wa magari ya Rally.
Maxine alikamatwa Desemba 12 nyumbani kwa Asad baada ya kaka wa marehemu kuripoti shambulio hilo kwa polisi mara baada ya kupewa taarifa na uongozi unaosimamia makazi hayo.
Kwa mujibu wa ripoti ya mahakama polisi walifika kwenye nyumba hiyo na kukuta marehemu akiwa ameshakimbizwa hospital, walifanikiwa kumkuta mwanamama huyo ambaye alionekana kama mtu aliyechanganyikiwa huku vifaa kadhaa vikiwa vimeangushwa sakafuni na kwenye ngazi.
Maxine ameachiliwa kwa dhamana ya shilingi za Kenya 100,000 huku kesi hiyo ikisubiri matokeo ya uchunguzi.