Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

CTI yataka sera nzuri ulinzi viwanda vya ndani

Leodegar Tenga CTI yataka sera nzuri ulinzi viwanda vya ndani

Sun, 11 Jul 2021 Chanzo: ippmedia.com

Hayo yalisemwa jana jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Shirikisho hilo, Leodgar Tenga, wakati akizungumza na wabunge wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira.

Tenga alisema viwanda vya ndani haviogopi ushindani wa bidhaa kutoka nje ya nchi, lakini bidhaa hizo zisipo dhibitiwa na kulipa kodi ipasavyo upo uwezekano wa kuviua viwanda vya ndani na kuwakosesha vijana wengi ajira.

Alisema mataifa yote duniani yanalinda viwanda vya ndani lengo likiwa ni kulinda ajira za wananchi wake hivyo serikali ya Tanzania inapaswa kuiga mataifa hayo.

“Hatuogopi ushindani na wala hatusemi kwamba kusiwe na ushindani na wenzetu wa nje kwa sababu bila ushindani viwanda vyetu vitabweteka lakini tunachoomba tusiviache tu bila ulinzi maana kupambana na maviwanda makubwa kazi kweli,” alisema Tenga.

Mbunge wa Bihalamuro Magharibi (CCM), Ezra John, naye aliunga mkono hoja ya kuvilinda viwanda vya ndani ambavyo vimeajiri mamilioni ya Watanzania na kwamba kufa kwake kutasababisha kuyumba kwa uchumi.

Alisema viwanda vya ndani kwa muda mrefu vimekuwa vikilalamikia utitiri wa kodi hivyo serikali inawajibika kuangalia namna bora ya kuzipunguza ili kuviondolea mzigo.

Ezra alisema wabunge na wadau mbalimbali wanapaswa kuangalia chanzo cha sheria hizo zinazolalamikiwa na kama bado zinapaswa kuendelea kuwapo au zifanyiwe marekebisho.

“Unaweza kukuta kuna mfanyabiashara alifanya makosa ikatungwa sheria ambayo inawabana watu wengi sasa lazima tujue sheria fulani inayolalamikiwa ilianzia wapi na kwasababu gani ili kama haina maana tena kwa wakati huu tuachane nayo,” alisema.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Erick Shigongo, alisema serikali inaendelea kuweka mazingira mazuri ya biashara, hivyo wenye viwanda nao wanapaswa kutimiza wajibu wao kwa kulipa kodi kwa uaminifu.

“Serikali hii inawalinda wafanyabiashara na wenye viwanda kwa kuweka sheria na sera nzuri, lakini nyinyi CTI muwakumbushe nao kwamba wanapaswa kuwa waaminifu kwa kutii sheria za nchi hii,” alisema.

Chanzo: ippmedia.com