Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Biashara United yaanza mikakati 'kuiua' Yanga

Mataso Ed Biashara United yaanza mikakati 'kuiua' Yanga

Fri, 28 May 2021 Chanzo: ippmedia.com

Biashara United ilitinga hatua hiyo baada ya kuwafunga Namungo FC mabao 2-0 kwenye mechi ya robo fainali sawa na ushindi ambao Yanga waliupata walipocheza na Mwadui FC mkoani Shinyanga.

Akizungumza na gazeti hili jana, Mwenyekiti wa Biashara United, Selemani Mataso, alisema wanatarajia kuingia kambini mapema wiki ijayo baada ya kocha wao, Patrick Odhiambo kurejea nchini akitokea kwao Kenya alipokwenda kuisalimia familia yake.

"Wiki ijayo ndio tutaanza mazoezi kwa ajili ya kujiandaa kukutana na Yanga kwenye mchezo wetu wa nusu fainali ya FA, lengo letu ni kuingia kwenye fainali ya mashindano hayo na tunawaomba mashabiki wetu wazidi kutuunga mkono ili tusonge mbele," alisema Mataso.

Kiongozi huyo alisema tayari kocha wao ameshabaini mapungufu ya kikosi chake na ameandaa mbinu mpya ili kuwaimarisha wachezaji wake kwa sababu wanahitaji kumaliza msimu huu na mafanikio.

Kuhusu suala la usajili alisema wana mpango wa kuongeza wachezaji ndani kwa ajili ya kuongeza nguvu kuelekea msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara na mashindano mengine watakayoshiriki.

"Baada ya kumaliza michezo yetu iliyobakia, kocha atatoa ripoti yake na baada ya kuipitia tutajua anahitaji wachezaji wangapi kwa ajili ya msimu ujao na anaacha wachezaji wangapi, tunaomba mashabiki wetu waendelee kuwa wavumilivu,” Mataso alisema.

Mwenyekiti huyo aliongeza kwa sasa wataendelea kupambana kwa kutumia wachezaji waliopo ambao wanaamini wamekuwa na msimu mzuri tofauti na misimu mingine iliyopita.

"Msimu huu umekuwa na ushindani sana, lakini tumefanikiwa kupambana na leo hii tuko katika nafasi za juu, ingawa malengo yetu yalikuwa ni kuwania ubingwa, naamini tutajiimarisha ili kufanya vizuri zaidi msimu unaofuata," aliongeza kiongozi huyo.

Biashara United yenye pointi 45 iko katika nafasi ya nne ikiwa imecheza mechi 30, imeshinda michezo 12, sare tisa na imepoteza michezo tisa.

Chanzo: ippmedia.com