OFISA Mtendaji Mkuu wa Klabu ya Simba Barbara Gonzalez amesema soka la wanawake linahitaji uwekezaji kama ilivyo kwa timu za wanaume kwa kuwa ushindani umeanza kuonekana.
Akizungumza na gazeti hili Dar es Salaam juzi, Barbara alisema uwekezaji ukifanyika kwenye ligi ya wanawake ushindani utazidi kuongeza na ligi itakuwa bora.
“Uwekezaji ukifanyika kwenye soka la wanawake ligi itakuwa bora zaidi, na kadiri miaka inavyosogea tayari tunaona namna timu zinavyoonesha soka la kuvutia, wadau waone hili na kujitokeza kuunga mkono,”alisema.
Alisema ni rahisi kwa wanawake kushiriki mashindano ya dunia kama tu kutakuwa na uwekezaji wa maana utakaozifanya timu kuibua vipaji vingi vyenye uwezo.
Alisema anaamini Tanzania imejaliwa vipaji vizuri na wengi amewaona katika kikosi chake cha Simba Queens namna baadhi yao walivyoibuka wachezaji bora.
Kuhusu mipango iliyopo kwa timu yake hiyo, alisema kwa kuwa msimu ujao watawakilisha nchi kwa mara ya kwanza kwenye michuano ya kimataifa wamedhamiria kuongeza bajeti ya kutosha kuwezesha timu hiyo kufanya vizuri zaidi.
Alisema wanataka kuweka historia ikiwezekana kuchukua taji la Ligi ya Mabingwa Afrika hivyo wataboresha kikosi chao kiwe bora kwa ushindani wa kimataifa.