Dar es Salaam. Mshambuliaji wa Stand United, Alex Kitenge 'amelia' kitendo cha Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kumpokonya mpira aliopewa baada ya kuifunga Yanga 'Hat-Trick'.
Kitenge amesema, baada ya mpira kumalizika alikabiziwa mpira huo sambamba na kupiga picha na mabosi wa Shirikisho, lakini baadaye viongozi hao waliuchukua na kutoa ahadi ya kumpa mwingine.
"Najisikia vibaya kwa sababu mpira huo ni haki yangu na sijui ni lini kocha atakwenda kufuata, nahitaji uwekwe kwenye rekodi ya kazi yangu ninazoendelea kufanya katika soka,” alisema Kitenge ambaye ni Mrundi mwenye asili ya Congo.
Ofisa Habari wa TFF, Cliford Ndimbo alisema Kitenge aliambiwa aende kuchukua mpira wake makao makuu ya shirikisho hilo, Karume jijini Dar es Salaam.
Kitenge, alifunga mabao hayo katika mchezo ambao Yanga ilishinda 4-3, mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliochezwa Jumapili iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Miongoni mwa sheria za Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), linatoa nafasi kwa mchezaji aliyefunga mabao zaidi matatu katika mchezo mmoja kupewa mpira uliotumika katika mechi husika.