Dar es Salaam. Mshauri mkuu wa chama cha ACT- Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad amemkaribisha katika chama hicho aliyekuwa mwanachama wa CCM, Bernard Membe lakini akimuonya asiwe na masharti.
Maalim Seif ametoa kauli hiyo leo Jumatano Machi 4, 2020 katika mahojiano yanayofanyika katika ofisi za kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) Tabata Relini jijini Dar es Salaam.
Maalim amtoa kauli hiyo siku chache baada ya Membe katika mahojiano na Mwananchi kudai kuwa alifukuzwa CCM kutokana na nia yake ya kutaka kupambana na mwenyekiti wa chama hicho, Rais John Magufuli kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2020.
Membe na makatibu wakuu wawili wastaafu, Abdulrahman Kinana na Yusufu Makamba walifikishwa mbele ya kamati ndogo ya udhibiti na nidhamu kujibu mashtaka ya kinidhamu.
Makada hao waliingia matatani baada ya sauti zao pamoja na za wanachama wengine watatu, kusambaa katika mitandao ya kijamii ikizungumzia kuporomoka kwa umaarufu wa chama hicho na uenyekiti wa Magufuli.
Makamba alisamehewa makosa yake wakati Kinana atakuwa chini ya matazamio kwa miezi 18, kipindi ambacho hataruhusiwa kugombea uongozi, wakati Membe amevuliwa uanachama na hivyo hataweza kutimiza ndoto yake ndani ya chama hicho.
Habari zinazohusiana na hii
- VIDEO: Maalim Seif asema bila ushirikiano wapinzani ngumu kushinda uchaguzi mkuu 2020
- VIDEO: Maalim Seif aweka wazi alichozungumza na Rais Magufuli
- Maalim Seif: Magufuli akutane na wapinzani wote kujadili uchaguzi huru na haki - VIDEO
- LIVE: MAALIM SEIF AKIWA MUBASHARA NDANI YA MWANANCHI KARIBU UTUFUATILIE
“Ya ndugu yangu Membe sisi chama chetu kitampokea yoyote atakayekuja mradi asije na masharti,” amesema Maalim Seif.
Alipoulizwa kuhusu kuomba msamaha ili arejee CCM, Maalim Seif angeweza kuomba msamaha tangu wakati wa Mwalimu Julius Nyerere akiwa Mwenyekiti wa CCM.
“Wakati huo kulikuwa na mawazo hayo kwamba tumewaonea hawa vijana tumewafukuza, kwamba wakiomba radhi tutawarejesha. Mimi nikasema sijasahau kitu CCM nirudi kutafuta nini? Kwanza watuondoe, kwamba nitarudi CCM No, never. Sitorudi CCM,” amesema.