Serengeti. Wataalam wa uchunguzi kutoka Jeshi la Wananchi la Tanzania (JWTZ) wameanza uchunguzi wa chanzo cha ajali ya ndege iliyoanguka jana Jumatatu Septemba 23, 2019 katika uwanja mdogo wa Ndege wa Soronera ndani ya Hifadhi ya Serengeti nchini Tanzania.
Katika ajali hiyo, Nelson Mabeyo aliyekuwa rubani wa ndege ya Kampuni ya Auric ambaye ni mtoto wa Mkuu wa Majeshi nchini Tanzania (CDF), Venance Mabeyo alifariki dunia akiwa na rubani mwanafunzi, Nelson Orutu waliokuwa pamoja.
Mkuu wa kanda ya Magharibi inayounganisha Hifadhi nane, Martin Loiboki akizungumza na Mwananchi kwa simu leo Jumanne Septemba 24, 2019 amesema wataalamu hao wamefika na wanaendelea na uchunguzi.
“Timu zote mbili zinaendelea na uchunguzi kila timu itatoa taarifa kwa waliowapa jukumu, sisi tunachofanya ni kuwapa ushirikiano ili kuhakikisha kazi hiyo inakamilika kwa wakati," amesema Loiboki
Bila kutaja idadi yao amesema wapo wengi na wamefika asubuhi ya leo na kuendelea na kazi na wale wa mambo ya anga ni wawili walianza jana Jumatatu.
Msimamizi wa kampuni ya Auric Air, Peter Kimaro amesema timu hiyo imeshafanya mahojiano na watu mbalimbali hapo ili kuwawezesha kupata taarifa sahihi za tukio hilo.
Habari zinazohusiana na hii
- VIDEO: Mtoto wa Mabeyo aliyekufa kwenye ajali ya ndege alitarajia kuajiriwa ATCL
- Mtoto wa mkuu wa majeshi Tanzania afariki ajali ya ndege
- Helikopta ya JWTZ yatua Serengeti kuchukua mwili wa mtoto wa Mabeyo
- Ndege yaanguka hifadhi ya Serengeti Tanzania, yaua wawili