Dar es Salaam. Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam nchini Tanzania, Muhashamu Yuda Thaddaeus Ruwa’ichi amesema anatamani kuona huduma aliyopewa yeye wakati akitibiwa wanapewa Watanzania wote.
Askofu Ruwa’ichi ameyasema hayo leo Jumatano Septemba 25, 2019 muda mfupi baada ya kuruhusiwa kutoka katika Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI).
SOMA ZAIDI: Askofu Ruwaichi afanyiwa upasuaji MOI
Usiku wa kuamkia Septemba 10, 2019, Askofu huyo alifanyiwa upasuaji wa MOI wa kuondoa damu kwenye ubongo baada ya kufikishwa katika taasisi hiyo akitokea Hospitali ya KCMC Moshi mkoani Kilimanjaro.
Kiongozi huyo wa kiroho, amesema huduma aliyopewa hospitalini hapo tangu alipowasili ilikuwa ya kutukuka na angetamani kila mwenye uhitaji aipate.
“Namshukuru Mungu kwa kunipa nafasi nyingine ya kuishi, nilikuja hapa nikiwa sijitambui hadi sasa najitambua. Nawashukuru madaktari na wauguzi kwa huduma.”
Pia Soma
- Geita yakwama kuanza kutoa chanjo ya watoto
- Rais Trump akalia kuti kavu, mchakato wa kumng’oa madarakani waanza
- Majaliwa atoa onyo kwa watendaji wa Serikali
SOMA ZAIDI: Jopo la madaktari kumjadili Askofu Ruwa’ichi leo
Profesa Jophesa Kahamba ambaye ni kiongozi wa jopo la madaktari bingwa waliomtibu Askofu Mkuu Rwa’ichi amesema wanashukuru tangu walipompokea (Askofu) mwili wake ulikuwa unakubali matibabu ndiyo sababu imeweza kupona haraka.
SOMA ZAIDI: Magufuli amjulia hali Askofu Mkuu Ruwa’ichi, aifariji familia ya CDF Mabeyo
Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mhashamu Eusebius Nzigilwa amesema alipata wasiwasi na akili yake ilikuwa inawaza kumpeleka nje ya Tanzania lakini walipowasiliana na Rais John Magufuli alikubali kutoa ndege ya kwenda kumchukua Moshi na kumpeleka MOI.
Amesema, “lakini muda wote nilikuwa na wasiwasi kwamba tutampeleka nje lakini ukweli ni kwamba MOI walituhakikishia ina vifaa vya kisasa na madaktari bingwa.”
Askofu Nzigilwa amewashukuru wale wote waliomhudumia (Askofu Ruwa’ichi).
SOMA ZAIDI: Magufuli amjulia hali Askofu Ruwa’ichi