Moshi. Askari wa kikosi cha usalama barabarani, William Mwakatage amefikishwa katika mahakama ya hakimu mkazi Moshi akikabiliwa na shtaka moja la kumnajisi binti wa miaka 15 ambaye ni mtoto wa askari mwenzake.
Mwakatage ambaye ni mwenyeji wa Mbeya amefikishwa mahakamani leo Ijumaa Februari 28, 2020 na kusomewa mashtaka ya ubakaji na mwendesha mashtaka wa Serikali Isaack Manguno mbele ya hakimu mkazi wa Moshi, Naomi Mwerinde.
Akisoma shtaka hilo, Manguno amesema mtuhumiwa huyo alitenda kosa hilo katika tarehe tofauti Oktoba na Desemba 25, 2019 eneo la kambi ya Polisi Moshi.
Amesema upelelezi wa shauri hilo umekamilika na kumuomba hakimu kupanga tarehe nyingine kwa ajili ya kusoma maelezo ya awali.
Baada ya kusomewa shtaka hilo, mshtakiwa huyo amekana na kuachiwa kwa dhamana baada ya kutimiza masharti.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Machi 17, 2020.
Habari zinazohusiana na hii
Tayari Mwakatage amefukuzwa kazi kutokana na kukabiliwa na tuhuma hizo.
Leo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Salum Hamduni amesema taratibu za kijeshi zimekamilika ikiwa ni pamoja na kumfukuza kazi.
Mwakatage alikamatwa na polisi Februari 15, 2020 ikiwa ni baada ya kupita zaidi ya siku 40 bila kuonekana kituo chake cha kazi baada ya kusambaa kwa taarifa za tukio hilo.