Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli amewataka Watanzania kutotishwa na janga la ugonjwa wa homa ya mapafu inayosababishwa na virusi vya Corona.
Amesema badala yake waendelee kuchapa kazi na kujenga uchumi huku wakizingatia tahadhari zote za kujikinga kuambukizwa ugonjwa huo kama zilivyotolewa na wataalamu.
Rais Magufuli amesema hayo leo Jumapili Machi 22, 2020 alipohudhuria Ibada ya Jumapili katika Kanisa la Mtakatifu Paulo wa Msalaba Jimbo Kuu Katoliki la Dodoma iliyoongozwa na Paroko wa Parokia hiyo, Padri Onesmo Wisi.
Katika salamu zake katika Ibada hiyo, Magufuli amesema kuwepo kwa ugonjwa wa corona isiwe sababu ya kutishana kiasi cha kumsahau Mungu.
Ametoa wito kwa Wakristo na waumini wa madhehebu mengine kumrudia Mungu ili aepusha janga hili, badala ya kumwacha shetani atawale.
Kiongozi mkuu huyo wa nchi amekemea tabia za baadhi ya watu wanaofanya mzaha juu ya ugonjwa huu ama kuwatia hofu wananchi kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii, na badala yake ametaka Watanzania waendelee kuchapa kazi huku wakizingatia tahadhari.
Habari zinazohusiana na hii
- Corona inavyogeuka ‘janga’ la uchaguzi kwa baadhi ya nchi
- Majaliwa awataja wanaoruhusiwa kutoa taarifa kuhusu corona
- Upulizaji dawa mabasi ya abiria kujikinga na corona wasuasua
“Tuendelee kuchapa kazi, tuendelee kuujenga uchumi wetu, hatuwezi kusalimu amri kwa ugonjwa huu wa Corona na kushindwa kumtegemea Mungu na tukashindwa kuendeleza uchumi wetu,” amesema Magufuli.
Amewashukuru viongozi wa Dini kwa kuungana na Serikali katika kuwahamasisha wananchi kuchukua tahadhari na ametoa wito kwa viongozi hao kuendelea kuliombea Taifa ili Mungu aepushe ugonjwa huo uliosababisha vifo vya watu zaidi ya 13,000 duniani kote hadi jana saa 5 usiku.