MICHUANO ya wavu ya ufukweni ya kitaifa inatarajia kufanyika leo na kesho katika fukwe za Mbalambwezi, Dar es Salaam.
Akizungumza na gazeti hili, Katibu Mkuu wa Chama cha Mpira wa Wavu,(Tava), Alfred Selengia alisema mashindano hayo yameandaliwa na Kamisheni ya Wavu wa Ufukweni, yatahusisha timu za wanaume na wanawake.
“Mashindano yataanza saa 2;00 asubuhi, na lengo ni kuwawezesha wachezaji kujivunia alama za kimataifa, ambazo zitawawezesha kushiriki michuano ya mikubwa duniani,” alisema Selengia.
Alisema pia mashindano hayo ambayo yanatambuliwa na mashirikisho ya mpira wa wavu Afrika-CAVB na lile la kimataifa –FIVB yatatumika kuchagua vikosi vya timu za taifa kwa ajili ya kufuzu michezo ya Olimpiki 2021 hatua ya pili.
Pia alisema mashindano hayo yatakuwa ya wachezaji wawili wawili na timu 29 zimejiandikisha, 16 za wanaume na 13 za wanawake.
Aidha, alisisitiza wachezaji kuwahi kulingana na ratiba ya mechi zao, kwani hakuna mchezo utakaorudiwa kwa sababu ya timu moja kuchelewa.