Ni wikiendi ya burudani iliyotawaliwa na hisia kwa wananchi wa Australia wakati wanatazamia kuchezwa kwa fainali za Australian Open 2022.
Baada ya miaka 42, raia wa Australia anafanikiwa kucheza fainali ya mashindano ya Australian Open. Si mwingine bali ni bingwa mtetezi wa Wimbledon na mchezaji namba 1 kwa ubora (wanawake) duniani, Ashleigh Barty.
Sehemu mbalimbali nchini humo zimepambwa kwa picha za Barty kuashiria siku kubwa na inayoweza kuweka historia kwa wananchi wake wakati ambapo, Barty atakuwa uwanjani leo usiku akichuana na Mmarekani, Danielle Collins kwenye fainali ya wanawake.
Japokuwa, Barty amekiri kuwa yeye huwa hafuatilii sana mitandao ya kijamii anapokuwa kwenye mashindano, ni dhahiri, shamrashamra za kuelekea mchezo wa fainali, anazisikia kwa watu wake wa karibu. Shauku inapamba moto!
Barty atawapa furaha wanayostahili wananchi wenzake au Collins atachafua hali ya hewa na kupeleka kombe Marekani?