Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Ukeketaji wageuzwa kipato

Babu Dfv Mmoja wa wazee akizungumza kwenye mkutano wa katika kijiji cha Mpakani, Sirari.

Tue, 30 Jul 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

"Na hii ndio sababu hasa ya kuendeleza ukatili huu. Ukeketaji huu ni maslahi. Ndio maana kabla ya msimu wa ukeketaji kuanza wanaandaa orodha ya majina ya watoto wa kike ambao watakuwa tayari kukeketwa. Wanapita kila ukoo kuhamasisha wapelekewe majina.

"Kwa hiyo, kabla ya ukeketaji kuanza wanakuwa na orodha ya watoto wangapi wanaokeketwa, na wengine wanapowakeketa wanawaozesha kwa wazee wenye kipato kizuri ili wapate fedha za kusaidia kutatua changamoto zao," anasema Rhobi.

Mkurugenzi huyo anasema zoezi la kuhamasisha watoto wapelekwe kukeketwa msimu wa ukeketaji unapokaribia, hufanywa kwa umakini mkubwa; katibu wa mila huzunguka na ngariba kuorodhesha majina ya wasichana.

"Na katika kila nyumba ambako wanafahamu kuna msichaka ambaye hajakeketwa, huwa wanaweka ulinzi wao kwa siri ili kuhakikisha haendi popote au kukimbia.

"Kwa mfano, sisi tuna nyumba ambayo tunaitumia kusaidia kuhifadhi wasichana ambao wanakimbia kukeketwa, tunaiita ‘nyumba salama’. Kikifika kipindi cha ukeketaji, wazee wa mila wanaweka ulinzi wao kuhakikisha wasichana hawaji katika nyumba hii.

"Huwa tunafanya kazi na bodaboda ambao huwa tunawaelimisha kwamba wanapoona mtoto anataka kukeketwa wasaidie kumtorosha, lakini kutokana na nguvu ya hawa wazee wa mila, kuna wakati na wao (bodaboda) huwa wanashindwa namna ya kuwaondoa wasichana kutokana na ulinzi mkali unaowekwa na hao wazee," anasema mkurugenzi huyo.

Rhobi anadai kuwapo vitisho dhidi yake kutoka kwa wazee wa mila kutokana na kusaidia wasichana wanaotoroka kukeketwa.

"Huwa wananiambia 'tutakuua', wanasema 'hata ukija na wenzako gari lenu litapinduka mfe' na wananitukana matusi, wanasema tunawaharibia kibarua chao," anadai Rhobi na kubainisha kuwa hadi sasa, kitu chake kina wasichana 104 kiliowapa hifadhi katika 'nyumba salama' baada ya kukimbia kukeketwa.

Hoja ya Rhobi kuhusu ukeketaji kugeuzwa 'duka' la ngariba na wazee wa mila, inaungwa mkono na Mwenyekiti wa Kijiji cha Mpakani, Kata ya Sirari, Julius Mwita, anayetaja malipo kwa ajili ya mtoto kukeketwa ndicho kikwazo kikubwa katika vita dhidi ya ukeketaji katika eneo lao.

"Zamani watoto wa kike wakikeketwa walikuwa wanavalishwa vitenge, baada ya kuona Jeshi la Polisi linafuatilia vitendo hivi, wanachanganya watoto wa kike na wa kiume kwenye ule msafara wa tohara, hivyo ni vigumu mgeni kufahamu, wasichana wengi wanaokeketwa ni wa umri wa balehe," anasema Julius.

Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk. Anna Henga anakosa adhabu iliyopo kisheria dhidi ya wanaokeketa wasichana, akiwa na hoja kwamba ni ndogo na inatolewa kwa waliotenda ukatili huo kwa watoto tu; hakuna adhabu iliyotajwa kisheria kwa anayekeketa mwanamke mwenye umri wa kuanzia miaka 18.

Inaporejewa Sheria ya Kanuni za Adhabu, Sura 16, kifunngu cha 69A(1) kinaelekeza: "Mtu yeyote ambaye ni mwangalizi, ana wajibu au usimamizi wa mtu yeyote mwenye umri wa chini ya miaka 18, akimtesa au akimtelekeza mtu huyo au akisababisha tohara kwa mwanamke au akimtahiri au kusababisha tohara hiyo ifanyike au kusababisha mtu huyo adhalilishwe, ateswe, au atelekezwe kwa namna ambayo itamsababishia maumivu au madhara kwa afya yake, pamoja na maumivu au kuharibu uwezo wake wa kuona, kusikia au kiungo chochote cha mwili au akili, atakuwa ametenda kosa la ukatili kwa mtoto.

Kifungu cha 169A(2) cha sheria hiyo, kinaelekeza kuwa mtu yeyote ambaye atapatikana na kwa kutenda kosa la aina hiyo kwa mtoto atawajibika kwa adhabu ya kifungo kisichopungua miaka mitano na kisichozidi miaka 15 au faini isiyozidi Sh. 300,000 au vyote kwa pamoja, na kuamriwa kulipa fidia ya kiasi kitakachoamuliwa na mahakama kwa yule aliyetendwa kosa hilo.

Dk. Anna anasema: "Tukiangalia madhara yanayowapata hao wasichana ikiwamo ugumba, kupata fistula, kupoteza watoto au kutokwa damu nyingi wakati wa kujifungua, unaona hakuna haja ya kufanya ukeketaji.

"Kuna haja kuunganisha nguvu kuanzia ngariba, serikali, asasi za kiraia na jamii kuwa na sauti ya pamoja kuondoa mgawanyiko uliopo wa wanaotaka ukeketaji uendelee na wanaotaka usiendelee.

"Sisi LHRC kwa kushirikiana na Mtandao wa Kupinga Ukeketaji Tanzania, tuliwahi kukutanisha wazee wa mila na viongozi wa dini. Kwa kweli mwaka ule ukeketaji ulishuka sana kwa sababu makundi hayo yana watu wenye nguvu katika jamii, wakisema 'hapana' na wananchi wanasema 'hapana'".

Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Kanali Maulid Surumbu, anasema jamii anayoongoza inaona ukeketaji si tatizo; ndio sababu hairipoti kwa vyombo vya dola matukio ya ukatili huo.

"Wanaripoti ubakaji na ulawiti, lakini tukio la msichana ameshikwa na kupelekwa kukeketa hawaoni kama ni tatizo na huwasikii wanakwenda kuripoti kwenye vyombo vya dola," anasema Kanali Surumbu.

Kiongozi huyo wa wilaya anasema kuwa hivi sasa wanaweka nguvu kubwa kuelimisha ngariba na wazee wa mila kuachana na ukeketaji.

"Kuna kipindi tuliandaa njia mbadala ya kusaidia wazee wa mila kupata kipato badala ya kutegemea ukeketaji, waliifuata kwa muda mfupi halafu baadaye wakarudia tena kufanya ukeketaji, bado tunaendelea kuwaelimisha," anasema Kanali Surumbu.

Mkuu wa Kituo cha Polisi Sirari, Rashid Chamwi, anasema jitihada za kudhibiti vitendo vya ukeketaji vinakwamishwa na mbinu mpya, hasa wazee wa mila kushirikisha ngariba kutoka nchi jirani.

"Tumepata malalamiko kwa wenzetu wa nchi jirani - Kenya, wanasema wasichana wanadhibitiwa kukeketwa huko kwao, wanaletwa nchini kwetu kuja kukeketwa, lakini hiyo si kwao tu, na sisi tukiwadhibiti huku wanakimbilia nchini jirani kwenda kufanyia huko. Ndio changamoto tunayotafuta mbinu ya kupambana nayo," anasema Chamwi.

Kwa mujibu wa Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dk. Dorothy Gwajima, mikoa yenye kiwango kikubwa cha ukeketaji kwa sasa ni Arusha (asilimia 43), Manyara (asilimia 43), Mara (asilimia 28), Singida (asilimia 20), Tanga (asilimia 19), Dodoma (asilimia 18), Iringa (asilimia 12), Morogoro (asilimia 10), Kilimanjaro (asilimia tisa), Njombe (asilimia saba), Pwani (asilimia tano) na Mbeya (asilimia tatu).

Waziri Dorothy anasema wizara inaendelea na utekelezaji mkakati wa kupunguza vitendo hivyo hadi asilimia tano ifikapo 2025, mwaka ambao ni ukomo wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live