Askari wa Jeshi la Polisi wametanda katika Uwanja wa Ruanda Nzovwe, jijini Mbeya kulipopangwa kufanyika maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani yaliyokuwa yameandaliwa na Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha).
Maadhimisho hayo yalikuwa yafanyike leo Jumatatu, Agosti 12, 2024, lakini Jeshi la Polisi kupitia kwa Kamishna wa Operesheni na Mafunzo, Awadh Juma Haji lilitangaza kuyasitisha baada ya kutilia shaka tukio hilo akieleza kutokuwa rafiki kwa mustakabali wa nchi.
Polisi ilitangaza uamuzi huo ukitanguliwa na barua ya Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kwenda Chadema ya Agosti 8, 2024 kukitaka kusitisha shughuli hiyo, kwani lugha za viongozi wa Bavicha zinahatarisha usalama na zinakiuka sheria.
Mwananchi imefika eneo la Uwanja wa Ruanda Nzovwe na kushuhudia idadi kubwa ya polisi wakiwa na bunduki pamoja na gari la washawasha, huku wakiwa wamezunguka kona zote za uwanja huo.
Pamoja na kuimarisha ulinzi huo, wananchi waliohitaji kukatiza eneo hilo kwenda katika shughuli zao wamekuwa wakihojiwa kabla ya kuruhusiwa kuendelea.