Kikongwe Tulivane Mkongea (85), mkazi wa Mtaa wa Idundilanga uliopo Wilaya ya Njombe mkoani hapa, ameuawa nyumbani kwake kwa kukatwa kichwani na kitu chenye ncha kali.
Hayo yamebainishwa jana Julai 21, 2024 na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Njombe, Mahamoud Banga alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.
Amesema Julai 20, 2024, saa 1 asubuhi, marehemu alikutwa nyumbani akiwa amefariki huku akiwa na jeraha kichwani linaloonyesha alikatwa na kitu chenye ncha kali.
Banga amesema sababu za kuuawa kwa marehemu huyo ni madai ya imani za kishirikina ambapo amekuwa akihusishwa na masuala hayo kwenye eneo analoishi.
Amesema anayedaiwa kufanya tukio hilo ni kijana anayefahamika kwa jina la Petro Mhenga ambaye amekuwa akifanya kazi ya kuchunga ng’ombe wa marehemu.
“Hawa tunawashikilia kutokana na mazingira kwa sababu mtu ameuawa, tukakuta wanafanya usafi wa nguo, mwili wa marehemu na eneo ambalo marehemu alikuwa ameuawa,” amesema Banga.