Aliyekuwa Spika wa Bunge, Job Ndugai, amedai kuwa aliwahi kumshauri Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, kukutana na Rais John Pombe Magufuli, ili kuzungumza mustakabali wa nchi.
Akizungumza jana Alhamisi, wilayani Kongwa, mkoani Dodoma, wakati wa mazishi ya Chibiriti Chiuyo, kada maarufu wa Chadema mkoani humo, Ndugai alisema, “niliwahi kumshauri mheshimiwa Mbowe, wakati akiwa mbunge wa Hai (Kilimanjaro), nami nikiwa spika wake, kwamba akutane na aliyekuwa rais wa Tanzania. Lakini alinikatalia.”
Ndugai ni mbunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika jimbo la uchaguzi la Kongwa, ambako mwili wa marehemu Chiuyo unatarajiwa kuhifadhiwa.
Wakati wa uhai wake, Chiuyo alikuwa miongoni mwa waasisi wa Chadema mkoani Dodoma na wilyani kwake Kongwa; akitoa mchango mkubwa wa kueneza na kukilinda chama hicho katika maeneo hayo.
Alifariki dunia Jumanne, na mazishi yake yalifanyika mchana wa jana. Akimnukuu Mbowe, ambaye alikuwa pia Kiongozi wa Kambi Rasmi ya upinzani bungeni, Ndugai alisema, “yule bwana aliniambia jambo hilo haliwezekani.”
Alisema, “nilipomuuliza Mbowe kwa nini haiwezekani?” Ndugai anasema, mwanasiasa huyo alijibu, “unawafahamu wale watu wangu. Hawatanielewa.”
Akiongea kwa kujiamini, Ndugai alisema, “siku moja, Mbowe akiwa mbunge, nilimuita ofisini kwangu. Nikamwambia, hivi kwa nini wewe usikae na rais aliyekuwapo (Magufuli). Wakazungumza baadhi ya haya mambo; si yatapungua.
“Kama kuna tatizo kubwa, mimi niko tayari kufanya mpango. Mkakutana na rais na mkazungumza. Akaniambia haiwezekani. Kwa nini haiwezekani?
Akasema, “wenzangu watanielewaje? Si unajua hawa jamaa zangu? Watanielewa vipi
Ndugai anasema, “lakini nikamwambia ukiwa kama kiongozi, hupaswi kuwa ndani ya boki, wewe na wafuasi wako wote. Lazima wewe kama kiongozi, lazima utoe kichwa nje; uwe unaangalia huko. Ukirudi ndani ya boki, unawaambia wenzio.
“Mkikaa wote ndani ya boki, hamtajua yanayoendelea huko nje. Akaniambi wapi! Hilo unalonishauri siyo kabisa.”
Akaongeza, “nashukuru leo hii, katoa kichwa nje ya boki.”
Hata hivyo, Ndugai anayejitapa kuwa alimshauri Mbowe kukutana na Magufuli, ndiye aliyemvua ubunge aliyekuwa mbunge wa Chadema, katika jimbo la Singida Mashariki, Tundu Lissu, katikati ya kuugulia majeraha ya risasi, aliyoshambuliwa akiwa bungeni mjini Dodoma.
Lissu alishambuliwa na wanaoitwa na serikali, “watu wasiojulikana,” nje ya nyumba yake, Area D, mjini Dodoma, tarehe 7 Septemba 2018.
Mara baada ya shambulio hilo, mwanasiasa huyo mashuhuri wa upinzani nchini, alikimbizwa nchini Kenya kwa matibabu na baadaye nchini Ubelgiji.
Ndugai alitangaza uamuzi wa kumvua Lissu ubunge wake, aliyoupata kwa jasho na damu katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, tarehe 28 Juni 2019.
Aliuambiwa mkutano wa Bunge wa jioni ya siku hiyo, kwamba amechukua uamuzi huo, kufuatia Lissu kutoonekana bungeni kwa muda mrefu bila yeye kuwa na taarifa ya maandishi; na kutojaza fomu ya tamko la mali na madeni.
Akiongea kwa hisia kali, Spika Ndugai alisema,“Septemba 2017, kwa sababu ambazo zinafahamika kwa kila mtu, mbunge wa Singida Mashariki, aliondoka hapa nchini kwa ajili ya matibabu nchini Kenya.
“Kufanya hadithi iwe fupi, mtakumbuka zaidi ya mwaka mmoja amekuwa akionekana kwenye vyombo vya habari vya kitaifa na kimataifa akifanya mihadhara mbalimbali.
“Lakini kwa muda wote huo, hajafika bungeni na hajawahi kuleta taarifa yeyote ile kwa Spika kuhusu mahali alipo na anaendeleaje; wala hajawahi kuleta taarifa kupitia kwa uongozi wake wa kambi au uongozi wa Bunge.”
Kufuatia hali hiyo, Ndugai alisema, Katiba ya nchi ipo wazi katika mambo ya aina hiyo, na pkwamba baadhi ya wabunge wameshapata matatizo kutokana na utoro kama huo wa Lissu.
Aliongeza, “…wa (utoro) kushindwa hata kuwambia Spika niko mahala fulani naendelea na jambo fulani hivi hakuna chochote, yaani kama kumdis-regard Spika kama hakuna chochote.
“Jambo la pili, wabunge wanatakiwa kujaza taarifa zenye maelezo ya mali na madeni kama Katiba inavyotaka. Tunatakiwa tujaze fomu mbili, na nakala inabaki kwa Spika.”
Alisema, “baada ya kuona kwenye kumbukumbu zangu hakuna fomu za Lissu, nilichukua jukumu la kupata uhakika wa jambo hili kwa Kamishena wa Tume ya Maadili na nilijibiwa kwa barua kwamba Lissu hajawasilisha na hawana taarifa zozote.”
Spika Ndugai alisema, kwa maana hiyo, Lissu hakuwa amejaa fomu na kwamba katika mazingira hayo, kifungu cha 37 kifungu kidogo cha 3 cha Sheria ya Uchaguzi kinamtaka kumtaarifu mwenyekiti wa NEC kuhusu suala hilo.
“Napenda kuwafahamisha kuwa nimemwandikia mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwamba jimbo la Singida Mashariki lipo wazi, alijaze kwa mujibu wa sheria zetu.
Nimefanya hivyo kwa sababu hizo mbili– kushindwa kuhudhuria mikutano ya Bunge kwa muda mrefu bila kutoa taarifa kwa Spika na kutotoa taarifa za mahali alipo na kugoma kutoa tamko la mali na madeni kama ibara ya 71 (1g) inavyotaka,” alieleza Ndugai.
Ni Job Ndugai huyo huyo, anayedai kumshawishi Mbowe kukutana na Magufuli, aliyewasakama wabunge kadhaa wa upinzani wakati wa uongozi wake, ikiwamo kuridhia uamuzi wa Prof. Ibrahim Lipumba wa kuwavua ubunge wabunge 8 kutoka Chama cha Wananchi (CUF), kinyume na taratibu.