Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) John Heche amesema ziara zinazofanywa na Viongozi waandamizi wa Chama hicho Kanda ya Ziwa zinakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo taarifa wanazoata kuhusiana na mipango haramu ya baadhi ya watu wanaopanga kuwafanya fujo kwenye mikutano yao
Heche ameambatana na Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho Tanzania Bara Tundu Lissu ameeleza hayo alipokuwa akizungumza na Wakazi wa eneo la Mganza, Wilayani Chato, Mkoa wa Geita.
Mbunge huyo mstaafu wa Tarime Vijijini amesema hatari ya msafara wao imeongezeka zaidi baada ya kufika Chato akidai ipo mipango hadi ya kutaka kuuwawa ili ioneshe watu wa Chato hawaitaki CHADEMA na hawamtaki Lissu.
Heche ameongeza kuwa, jambo hilo halijawastua na halikuwatisha kuingia Wilaya hiyo na ndio maana wameendelea kufanya mikutano kama ilivyopangwa.
"Sasa sisi tukasema, wewe unamuona Lissu huyu hapa, ni mtu aliyepigwa risasi 16, Haya Mimi binafsi niliwahi kuzungumza hapa, niliwaambia kwamba ukiona natetemeka Mimi ni baridi, Mimi sijawahi kumuogopa mtu hata awe na mapembe yanatoboa kule, kwa sababu Duniani hapa tumeumbwa mara moja na tutakufa mara moja," amesema Heche.
Amesema kila mmoja anapaswa kuondokana na nidhamu ya woga kwakuwa nchi hii (Tanzania) ni ya wote na kwamba kinachotokea sasa ni uwepo wa utawala wa watu waovu waliokaa madarakani kwa miaka 63.