Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere (Mwalimu Nyerere Foundation), Mzee Joseph Butiku, amekemea tabia ya baadhi ya watu kumchangia fedha Rais Samia Suluhu Hassan, kwa ajili ya kuchukua fomu ya kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2025, akisema ni rushwa.
Mzee Butiku ametoa kauli hiyo katika ufunguzi wa kongamano la miaka mitatu ya Taasisi ya Kizalendo Tanzania Patriotic Organisation (TPO), jijini Dar es Salaam.
“Sasa hivi CCM kinachanga mnafanya nini hiko? Niwaambie mimi ni mzee mmeanza kumchangia kabla ya uchaguzi wa mwaka kesho wanachanga Leo hiyo ni rushwa tu. Mkitaka leo kuniripoti Mzee Butiku amesema kumchangia Rais ni rushwa mseme,” amesema Mzee Butiku.
Mzee Butiku amesema tabia ya kumchangia wagombea hela itaongeza rushwa kwani ikifika wakati wa chaguzi watu watalazimika kuchanga hela kwa wagombea wanaowahitaji ili waweze kushinda.
Mwanasiasa huyo mkongwe nchini Tanzania, amesema aliwahi kutofautiana na aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tatu, Hayatu Benjamin Mkapa kuhusu suala la kutoa rushwa kwa wananchi ili wamchague.