Serikali imesema katika kipindi cha mwaka 2024/2025, imepanga kutumia Sh Bilioni 30 kuimarisha huduma za watoto wachanga katika hospitali 100 nchini.
Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Stela Fiyao, aliyehoji kuhusu mpango wa serikali kupeleka mashine za watoto njiti katika hospitali zote za mikoa na wilaya, Naibu Waziri wa Afya, Dk Godwin Mollel, amesema:
“Kwa mwaka wa fedha 2023/24, Serikali imepeleka vifaa vya kusaidia Watoto njiti kwenye vituo vya kutolea huduma za afya 241 vyenye jumla ya thamani ya Sh bilioni 2.6 hadi kufikia Machi 2024.
“Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2024/2025 serikali imepanga kutumia Sh bilioni 30 kuimarisha huduma za watoto wachanga katika hospitali 100 kwa kujenga wodi maalum (NCU) za watoto wachanga, watoto njiti na ununuzi na usambazaji wa vifaa tiba ikiwemo mashine za kuwasaidia watoto wachanga njiti kupumua.”