Wataalamu wa uchunguzi wa virusi na vimelea vya magonjwa wamebaini chanzo cha virusi vya homa ya nyani, maarufu ‘Mpox’ ni pamoja na panya wa msituni na si nyani pekee.
Taarifa hizo zinatolewa baada ya miaka mingi kuaminika kuwa chanzo pekee cha homa hiyo ni nyani wanaopatikana Afrika ya Kati na Magharibi.
Aina mpya ya homa ya nyani imesababisha mamia ya vifo katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) na imeenea katika maeneo ya Afrika ya Kati, Mashariki na mabara kadhaa duniani.
Hayo yamebainishwa Agosti 24, 2024 na Mwenyekiti wa Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala, Profesa Hamis Malebo wakati akizungumza katika mdahalo ulioendeshwa na Wizara ya Afya kupitia mtandao wa X uliokuwa na mada isemayo; ‘Elimu kuhusu ugonjwa wa Mpox, Jikinge; iweke Tanzania salama dhidi ya Mpox.’