Serikali imesema kuanza kutekelezwa kwa Bima ya Afya kwa wote itakuwa suluhisho la kudumu la kurahisisha upatikanaji wa huduma za afya kwa makundi yote nchini ikiwemo wanafunzi.
Kauli hiyo imebainishwa na Naibu Waziri wa Afya, Dk Godwin Mollel leo Mei 10,2024 Jijini Dodoma wakati akijibu swali Namba 305 kutoka kwa Mbunge wa Sikonge,Joseph Kakunda aliyeuliza Je, Serikali haioni haja ya kuwalipia wanafunzi gharama za matibabu wanapougua wakiwa shuleni.
Aidha,Dk Mollel amesema kuwa Serikali imeweka utaratibu maalum kupitia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, ambapo wanafunzi wanajiunga Bima ya Afya kwa makundi kupitia shule wanazosoma kwa kuchangia shilingi 50,400 kwa mwaka.
“Mpango huu wa Bima ya afya kwa wanafunzi unawasaidia kupata huduma za matibabu wakiwa masomoni na wakati wa likizo”, amesema Dk Mollel.
Hata hivyo Dk Mollel amewakumbusha watanzania wote kuwa utaratibu wa bima ya afya kwa wote ni kuchangiana huduma za matibabu na wala sio kusadiana au msaada.