WACHEZAJI wa kulipwa kutoka klabu vya gofu kote nchini watashiriki mashindano ya gofu yanayotarajiwa kufanyika Aprili 30 na 31 mwaka huu katika viwanja vya Lugalo, Dar es Salaam.
Aidha, wachezaji wa ridhaa wa mchezo huo zaidi ya 100 watasindikiza michuano hiyo ya siku mbili.
Akizungumza Dar es Salaam juzi, Ofisa Habari wa Klabu ya Gofu Lugalo, Kapteni Selemani Semunyu alisema mashindano hayo ya kipekee yanatarajiwa kuwa na upinzani mkali
“Lugalo kama kawaida yetu ni klabu kubwa ambayo tunapenda kuandaa mashindano kila mara, hivyo Aprili 30 na 31 tutakuwa na mashindano ya wachezaji wa kulipwa ambao watasindikizwa na wachezaji wa ridhaa,” alisema Semunyu.
Naye Frank Mwinuka ambaye ni miongoni mwa wachezaji wa kulipwa watakaoshiriki michuano hiyo, alisema amejiandaa vema na anachosubiri ni muda wa mashindano kufika.
“Lugalo ni nyumbani kwetu, uwanja naujua vizuri na kwa mazoezi niliyofanya nina amini nitafanya vizuri,” alisema Mwinuka.