Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

VITA YA KAGERA: Yusufu Lule aunda Serikali ya mpito -23

34311 Pic+kagera Tanzania Web Photo

Tue, 1 Jan 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Baada ya Jiji la Kampala kuangukia mikononi mwa majeshi ya Tanzania, hali haikutulia kama ilivyotazamiwa. Usiku wa Jumanne ya Aprili 10 kuamkia Jumatano ya Aprili 11, 1979, maelfu ya wanajeshi wa Tanzania walikuwa wakivinjari katika jiji la Kampala.

Vikosi kadhaa vya Brigedi ya 208 iliyokuwa chini ya Brigedia Mwita Marwa vilikuwa kusini mwa mji huo. Brigedi ya 207 ya John Butler Walden (Black Mamba) ilikuwa upande wa magharibi mwa jiji, na Brigedi ya 201 chini ya Brigedia Imran Kombe ilikuwa imeweka kizuizi upande wa kaskazini.

Hadi mapambazuko ya Jumatano ya Aprili 11, 1979, wanajeshi wa Tanzania wakawa katika kila kona ya kila barabara iliyoingia katika Jiji la Kampala, ikiwa ni pamoja na barabara iliyoelekea Jinja. Askari yeyote wa Idi Amin ambaye alikuwa amesalia katika mji wa Kampala sasa alikuwa anawindwa na waliopatikana waliuawa.

Mapema Jumatano asubuhi, wapiganaji wa ukombozi wa Uganda, pengine kutokana na wengi wao kulewa usiku wa jana yake, walianza kuwaghasi raia waliokuwa wakipita na magari yao mitaani. Lakini kiongozi wao, Kanali David Oyite Ojok alilazimika kuingia kwenye studio za Redio Uganda kuwatangazia waache kuwasumbua watu.

Kanali Ojok alitaka kutimiza ndoto yake ya kuwatangazia Waganda kuwa sasa wako huru dhidi ya Iddi Amin. Lakini Profesa Yusuf Kironde Lule, kiongozi wa Umoja wa Kuikomboa Uganda (UNLF), akitambua ukaribu uliokuwapo kati ya Kanali Ojok na Dk Milton Obote, alihofia kuwa Ojok angetangaza kuwa Obote amerejea madarakani nchini Uganda.

Kanali Ojok alipokuta simu iliyokuwa ikifanya kazi katika studio za Redio Uganda, aliitumia kwa kupiga simu mbili jijini Dar es Salaam. Simu moja alimpigia Rais Julius Nyerere na simu ya pili alimpigia Obote. Ojok alikuwa amemwahidi Obote kuwa angempigia simu mara atakapokuwa amefika Kampala, na sasa alikuwa anatimiza ahadi yake.

Mwalimu Nyerere hakuwa ofisini kwake wakati Kanali Ojok akimpigia simu, lakini Ojok akaacha ujumbe kwa ofisa usalama aliyepokea simu hiyo kwamba Kampala imedhibitiwa. Alipozungumza na Obote, Kanali Ojok alimwambia kuwa amenuia kutangaza kukombolewa kwa Kampala “kwa jina la UNLF”. Obote alimjibu kwamba hilo ni jambo jema.

Ingawa Kampala ilikuwa imeshakombolewa kutoka kwa Iddi Amin, milio ya risasi ya hapa na pale ilikuwa ikisikika mitaani na wakati mwingine milio ya mabomu nayo ilisikika. Pamoja na yote hayo, mafundi mitambo wa Redio Uganda walifika kazini na kuendelea na kazi zao kama kawaida.

Ojok aliamua kutoa matangazo yake kupitia Redio Uganda. Alitangaza kuwa utawala wa Amin nchini humo umeondolewa na kwamba sasa Kampala ilikuwa mikononi mwa UNLF.

Ojok alinukuliwa na jarida la Tarehe Sita akisema: “Tunauomba umma wa Waganda kuamka na kuungana pamoja kuwaondoa kabisa wauaji wachache waliobakia.”

Aliendelea kusema, “Tunawaomba wapenda amani wote wa dunia hii kuwaunga mkono wakombozi wa Uganda na waulaani utawala uliopita wa kifashisti.”

Ojok aliwataka raia wa Kampala kuwa watulivu na kisha akawataka askari wa Iddi Amin “…popote walipo nchini Uganda wajisalimishe mara moja.”

Ingawa alitangaza hayo, mjini Dar es Salaam Profesa Lule ambaye alikuwa akiyasikiliza matangazo hayo ya Kanali Ojok kupitia Redio Tanzania Dar es Salaam (RTD), ambayo iliyarudia matangazo ya Ojok ya Redio Uganda, hakuyapenda sana—huenda ni kwa sababu hakusikia jina lake likitajwa katika matangazo yenyewe. Aliamini kuwa huu ndio wakati wake wa kusikika—wakati wa kihistoria katika maisha yake na historia ya Uganda.

Kiuhalisia, Profesa Lule alikuwa hotelini mjini Dar es Salaam wakati Ojok na wengine wakiwa katika uwanja wa mapambano dhidi ya utawala wa Iddi Amin kwa kipindi cha miaka kadhaa na sasa walifanikiwa kupigana hadi kuitwaa Kampala.

Profesa Lule aliamua kuandaa tangazo lake mwenyewe ambalo lingetolewa na Redio Uganda. Tangazo hilo lilirekodiwa kwenye mkanda wa kaseti mjini Dar es Salaam na baadaye likatumwa Kampala, Uganda kwa ajili ya Redio Uganda. Ingawa hivyo, tangazo lililonukuliwa na vyombo vya habari vya kimataifa ni lile la Kanali Ojok na si lile la Profesa Lule.

Katika mkanda wa kaseti uliorekodiwa Dar es Salaam na kupelekwa Kampala, kwa mujibu wa jarida la Summary of World Broadcasts: Non-Arab Africa la Ijumaa ya Aprili 13, 1979, Profesa Lule alisema: “Najisikia heshima na faraja kuwatangazia muundo wa Serikali ya mpito kwa nchi yenu (Uganda). Serikali yenu itakuwa kama ifuatavyo....”

Baada ya kujitaja mwenyewe kama Rais wa Serikali ya mpito ya Uganda na mawaziri wake aliowateua akiwa mjini Dar es Salaam, Profesa Lule alitaka kuwapo na utawala wa sheria, kisha akaahidi kuwa utafanyika Uchaguzi Mkuu nchini Uganda “mapema kadri hali itakavyoruhusu”.

Miongoni mwa waliotajwa katika baraza lake la mawaziri ni pamoja na Sam Sabagareka, Otema Alimadi, Paulo Mwanga, Dk Arnold Bisasi, A. Biararuha, Mathias Ngobi, Profesa Asavia Wandira (Elimu), Dani Wadada Nabudere (Utamaduni na Maendeleo ya Jamii), George Wilson Kanyeihamba (Sheria) na Luteni Kanali William Omaria.

Lakini siku moja baada ya matangazo hayo Iddi Amin alijibu. Katika matangazo yake Amin alimjibu Ojok na si Profesa Lule. Amin alikuwa akizungumza kutokea mahali fulani magharibi mwa Uganda. Inawezekana alikuwa akizungumza kupitia kituo fulani cha idhaa ya nje ya Redio Uganda au kwa kutumia magari ya matangazo ya redio aliyoyanunua kwa gharama akiwa madarakani.

Kwa mujibu wa gazeti la The Washingtong Post la Aprili 12, 1979 chini ya kichwa cha habari Uganda Capital Cuptured, Iddi Amin alinukuliwa akisema: “Mimi Rais Iddi Amin Dada wa Jamhuri ya Uganda, napenda kukanusha matangazo yaliyotolewa na aliyekuwa Luteni Kanali wa jeshi, Oyite Ojok, kwamba eti Serikali yangu imepinduliwa na eti Serikali ya uasi imeundwa Uganda...” Nini kilitokea?

Soma zaidi: VITA YA KAGERA: Msuya ashangilia kuiteka Kampala -22

Itaendelea kesho



Columnist: mwananchi.co.tz