Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

VITA YA KAGERA: JWTZ waingia Uganda kwa mashua-6

31758 Pic+kagera Vita ya Kagera

Sat, 15 Dec 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Usiku wa Jumanne ya kuamkia Novemba 15, 1978, kikosi cha kwanza cha askari wa Tanzania, kikiwa chini ya Luteni Kanali Benjamin Noah Msuya, kilivuka Mto Kagera kwa mashua ndogo na kuingia ng’ambo ya pili.

Hadi kufikia wakati huo (wa kuvuka mto), zaidi ya Watanzania 1,000 walikuwa wameuawa, alisema Msuya katika mahojiano na gazeti The Monitor la Uganda la Jumamosi ya Mei 3, 2014 nyumbani kwake Kunduchi, Dar es Salaam.

Msuya aliongoza batalioni ya 19 ya JWTZ iliyokuwa chini ya Brigedi ya 208 iliyoongozwa na Brigedia Jenerali Mwita Marwa. Kazi yake ilikuwa ni kuivamia na kuitwaa Kampala, lengo ambalo hatimaye lilifikiwa Jumanne ya Aprili 10, 1979.

Baada ya kufanikiwa, Luteni Kanali Msuya akaitawala Kampala kama meya wake na pia kama rais wa Uganda kwa siku tatu hadi nchi hiyo ilipompata Yusuf Kironde Lule kuwa rais.

Alfajiri ya Jumapili ya Novemba 19, Luteni Kanali Msuya alituma kikosi kingine cha askari kwenda ng’ambo ya Mto Kagera, kikitumia mashua nyingine ndogo. Huko walishangazwa sana kuona uporaji na mauaji yaliyofanywa na askari wa Idi Amin.

Miili ya Watanzania waliouawa na majeshi ya uvamizi ilikuwa imeshaanza kuoza. Kikosi hicho kiligundua kuwa miili mingine ilikuwa imekatwa viungo, ishara kwamba wengi wao waliteswa kabla ya kuuawa.

Serikali ya Tanzania ilisema kiasi cha wakazi 40,000 walivuka Mto Kagera kukimbia majeshi ya Uganda, wakiacha kiasi cha raia kati ya 5,000 na 10,000 wakihofiwa kuuawa.

Miongoni mwao, kwa mujibu wa gazeti la Serikali la Daily News, walikuwako Watanzania 485 waliopelekwa gereza la Mutukula upande wa Uganda, ambako waliuawa kwa kulipuliwa kwa baruti.

Habari iliyoandikwa na John Darntonnov kwenye gazeti The New York Times la Alhamisi ya Novemba 23, 1978 inasema katika maeneo yaliyovamiwa na majeshi ya Idi Amin, hasa ya biashara, “kitu pekee chenye uhai kilichoonekana (baada ya uvamizi) ni mbwa mweusi aliyekonda” baada ya raia Watanzania wengi kuyakimbia majeshi ya Idi Amin.

Maduka yote, kwa mujibu wa The New York Times, yaliporwa.

“Katika duka moja lililoporwa, kilichokuwa kimesalia dukani hapo ni picha ya harusi ya mmiliki wa duka, Zaharan Salum na bibi harusi wake, ambayo ilikuwa inaning’inia ukutani,” liliandika gazeti hilo.

Kati ya ng’ombe 12,000 waliokuwa ranchi ya Narco, ni ng’ombe 100 tu walisalia baada ya wengine kuporwa. Wamiliki wa ranchi hiyo, ambao ni raia wa Australia, hawakuonekana baada ya uporaji huo na ilihofiwa kuwa nao waliuawa. Kiwanda ha sukari cha Kagera na shamba la miwa, viliteketezwa.

Doria ya Luteni Kanali Msuya ilifika hadi mpakani mwa Uganda Jumatano ya Novemba 22. Kwa wakati wote huo askari wa Amin hawakuonekana. Lakini doria hiyo ilipofika eneo la Minziro, iliona kiasi cha askari 30 wa Amin na vifaru viwili vikiwa eneo la kanisa. Askari hao wa doria hawakufanya shambulio lolote bali walirudi hadi Kyaka.

Ijumaa ya Novemba 24, vikosi kadhaa vya JWTZ, vikiongozwa na mabrigedia watatu; James Luhanga, Mwita Chacha Marwa na Silas Mayunga vikawa vimetanda kuzingira maeneo yaliyotekwa.

Siku hiyo hiyo daraja la dharura la Mto Kagera likaanza kujengwa kwa ajili ya kuvusha vifaru na zana nyingine za kivita. Kazi hiyo ilikamilika na siku iliyofuata na zana za kivita zikaanza kuvushwa.

Wakati daraja la dharura likijengwa, Rais Nyerere alizuru eneo hilo. Ingawa awali makamanda wa JWTZ walitaka kumzuia. Akiwa uwanja wa vita, alitumia darubini kutazama wapiganaji wa Amin wakiwa vilimani, umbali wa kilometa kumi kutoka mpakani, tayari kuishambulia Tanzania.

Ziara hiyo ya Nyerere ilimshawishi kukubaliana na makamanda wa JWTZ kuwa eneo la Kagera haliko salama na kwamba ili usalama uwepo, ilikuwa ni lazima jeshi la Tanzania livuke mpaka.

Usiku wa Jumapili ya Novemba 21, 1971 askari wa Tanzania walivuka mpaka na kuingia Uganda. Kikosi cha kwanza kilisaidiwa na vifaru na kiliongozwa na Luteni Kanali Salim Hassan Boma.

Vikosi kadhaa vilijizatiti maeneo ya misitu kuzunguka mji wa Mutukula. Kabla ya kupambazuka, kikosi kimojawapo kilichoongozwa na Luteni Kanali Salim Hassan Boma, kikisaidiwa na vifaru, kilitembea katika barabara kuu ya kuelekea Mutukula. Hii ilikuwa ni mbinu ya kuwavuta adui na ilifanikiwa.

Wakati majeshi ya Idi Amin yakifuatilia nyendo za kikosi cha Luteni Kanali Boma kilichokuwa mbele yao, yalishtukiwa yakishambuliwa na kikosi kingine cha JWTZ kutoka nyuma yao. Kwa jinsi askari wa Idi Amin walivyopagawa, walilazimika kukimbia na kutelekeza silaha zao.

Kwa njia hiyo JWTZ ikajipatia silaha mbalimbali kuanzia vifaru hadi bunduki za kawaida. Katika mapambano hayo, kikosi cha Luteni Kanali Boma kilipoteza wanajeshi watatu na wengine kadhaa kujeruhiwa. Hata hivyo, bila ujasiri huo ilikuwa ni vigumu kuvunja ngome ya jeshi la Uganda katika vilima vya eneo hilo.

Kwenye mapigano ya Mutukula, idadi kubwa ya raia waliuawa.

“Kila kitu kiliharibiwa na kila kilichokuwa na uhai kiliuawa,” imeandikwa katika kitabu cha War in Uganda.

“Mabuldoza yalifukia nyumba zote za udongo. Vikongwe ambao hawakuweza kukimbia waliuawa kwa kupigwa risasi. Kufikia mchana (Jumatano ya Novemba 22, 1978) Mutukula haikuwapo tena isipokuwa kwenye ramani.”

Jeshi la Tanzania “lilianza kulipiza kisasi kwa namna isiyotofautiana na ile ya Idi Amin” wakati akiteka eneo la Kagera.

Habari za ushindi wa kuitwaa Kagera zilimfariji Mwalimu Nyerere, lakini inasemekana, hakufurahishwa na habari za mauaji yaliyofanywa na jeshi lake.

Baadaye Nyerere alitoa amri ya maandishi kwa jeshi lake litofautishe jeshi na raia na mali zao. Vyovyote iwavyo, ushindi wa kwanza ukawa umepatikana kwa kuikomboa Mutukula.

Soma zaidi: VITA VYA KAGERA: Nyerere, Samora wakubaliana kumpiga Idi Amin-5

Siku JWTZ ilipovuka mpaka, Serikali ya Uganda ilitangaza kuwa wanajeshi zaidi ya 1,000 wa Tanzania wameingia maili 100 ndani ya Uganda na kuteka miji mitatu ya Kyotera, Kakuto na Kalisizo.

Itaendelea kesho



Columnist: mwananchi.co.tz