Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

VITA VYA KAGERA : Utekaji wa kwanza wa ndege kielektroniki duniani wafanywa na Jeshi la Wananchi-16

33321 Pic+kagera Tanzania Web Photo

Wed, 26 Dec 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Katika toleo lililopita tuliona wanajeshi wa Tanzania walivyopata shida katika mji wa Lukaya kiasi kwamba waliamua kuutangaza kuwa nI sehemu ya maafa kwa Watanzania. Eneo la Sembabule nalo lilileta changamoto nyingine kubwa kwa askari wa JWTZ.

Katika toleo hili tutaona namna mabadiliko ya uongozi katika Brigedi ya 205 yalivyoleta tofauti kubwa na hatimaye JWTZ ikaibuka mshindi. Katika kuipanga upya Brigedi ya 205, Brigedia Herman Lupogo aliondolewa akaingia Brigedia Muhidin Kimario. Endelea…

HATA baada ya Tanzania kuiteka Masaka, Idi Amin alisikika katika Redio Uganda akijigamba kuwa Watanzania walikuwa wanazingirwa. Kusikia hivyo, Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) lilianza kuchunguza taarifa zao.

JWTZ iligundua kulikuwa na kikosi kizima chini ya kanali kilichoitwa Tiger Regiment kilichokuwa Mubende, katikati ya Masaka na Mbarara.

JWTZ haikuwa imeweka mpango wowote wa kukishughulikia. Kwa kuzingatia alichosema Amin, wachambuzi wa masuala ya kijeshi wakaamini kuwa huenda kikosi hiki kilikuwa kinaelekea kusini ambako kingeanza kuwazingira Watanzania.

Brigedi ya 205 chini ya Brigedia Herman Lupogo iliamriwa kuondoka Masaka kwenda kukabiliana na Tiger Regiment. Haukupita muda mrefu hadi Lupogo alipogundua kilipo kikosi hicho ambacho hadi sasa kilikuwa kimeongezewa nguvu na wapiganaji kutoka Kituo cha Mafunzo ya Kijeshi cha Kabamba na kilijichimbia eneo la Sembabule.

Vita kali ambayo ilidumu kwa wiki tatu ikaanza. Tanzania ilipigana kutwaa eneo moja, lakini wakashtukia kesho yake eneo hilo limetwaliwa tena na majeshi ya Idi Amin.

Hata baada ya kutwaa tena eneo ambalo walinyang’anywa na askari wa Amin, wanajeshi wa Tanzania walikuwa wakikuta maiti za Watanzania katika eneo waliloliteka upya.

Baadaye wapiganaji wa Tanzania wakajikuta wakiogopa na kuvunjika moyo. Vikundi na vikosi vidogo sasa vilikuwa vikikimbia wakati majeshi ya Amin yakishambulia.

Katika kuipanga upya Brigedi ya 205, Brigedia Lupogo aliondolewa katika kikosi hicho na akaletwa Brigedia Muhidin Kimario. Awali Kimario alionekana ni mwanasiasa zaidi kuliko mwanajeshi. Wakati mmoja alikuwa mbunge wa Moshi na kabla vita havijaanza alikuwa mkuu wa Mkoa wa Mwanza.

Alipowasili Sembabule aliikuta Brigedi ya 205 ikiwa shaghalabaghala. Kiasi cha askari 20 au zaidi wa brigedi hiyo walikuwa wameuawa. Wengine walikata tamaa. Makabidhiano ya brigedi kutoka kwa Lupogo kwenda kwa Kimario yalifanyika wakati brigedi ikiwa inashambuliwa na askari wa Amin.

Mara moja Kimario aliwaita askari wake na kuwaahidi kuwa kila atakapotoa amri ya kwenda kwenye mapambano atakwenda nao bega kwa bega.

Kimario aliamua kuacha mbinu za matumizi ya vitengo vidogo vidogo katika brigedi iliyokuwa ikitumiwa na Brigedia Lupogo na badala yake akaamua kuipeleka brigedi nzima mbele kushambulia.

Mbinu ya Kimario ilizaa matunda. Ari mpya ikarudi kwa wapiganaji wa Brigedi ya 205. Ingawa mapigano yalidumu kwa muda fulani, hatimaye Tiger Regiment ikaelemewa. Katika mapigano ya mwisho ambayo katika hayo kikosi hicho cha Idi Amin kilikimbia, brigedi ya Kimario iliua askari 25 wa Amin.

Wakati wote wa mapigano ya Lukaya na Sembabule yakiendelea, Rais Nyerere alikuwa akienda Bukoba mara kwa mara kupata picha halisi ya kinachoendelea vitani badala ya kukaa ofisini na kutegemea taarifa alizokuwa akiletewa. Baada ya ziara yake moja alirejea Dar es Salaam na hofu—ushiriki mkubwa wa Libya katika Vita ya Kagera.

Sasa Nyerere akaona kuwa ushiriki wa moja kwa moja wa Libya katika vita ya Uganda ni uhalali tosha wa Tanzania kumchakaza Idi Amin. Wapiganaji waliokuwa wakikusanywa na vikundi vinavyompinga Amin havikuwa vimefikia matumaini aliyokuwa nayo Nyerere.

Kwa kukasirishwa na kitendo cha kiongozi wa Libya, Muammar Gaddafi kuliingiza jeshi lake nchini Uganda dhidi ya Tanzana, Nyerere akaiamuru JWTZ kuingia Kampala na kuuteka mji huo.

Wakati huu silaha zaidi na wanajeshi zaidi kutoka Libya walikuwa wakiingia Uganda. Ndege za kijeshi zilizotengenezwa Urusi, Tupelev-22, zilikuwa zikiruka kutoka uwanja wa jeshi wa Nakasongola na kwenda kurusha mabomu vilikokuwa vikosi vya Tanzania kusini mwa Uganda.

JWTZ, kwa kuona ndege za Libya zikawa zinaingia Uganda mara kwa mara, ikaamua kutafuta namna ya kuziteka. Hapo ndipo utekaji wa kwanza wa kielektroniki duniani ulifanyika. Kabla ya hapo hakukuwahi kutokea utekaji mwiingine wa aina hiyo mahali popote duniani.

Usiku wa manane, wanajeshiwa JWTZ wakiwa Mwanza, walisubiri hadi pale walipoona kwenye rada ndege mojawapo ikielekea Entebbe, upande wa Uganda, karibu na Ziwa Victoria.

Waliwasiliana na rubani wa ndege hiyo na kujitambulisha kwake kwamba wao ni waongozaji wa ndege katika Uwanja wa Entebbe na kumwonya kuwa uwanja huo, Entebbe, unashambuliwa vikali na wanajeshi na kwa sababu hiyo haingefaa atue kwenye uwanja huo.

Wasiwasi mkubwa ulimpata rubani huyo kiasi kwamba alilazimika kuomba ushauri. Wanajeshi wa JWTZ wakamshauri kuwa uwanja wa ndege ulio karibu zaidi ni ule wa Mwanza na kwamba kwa sasa ni salama zaidi kutua kwenye uwanja huo.

Rubani alijaribu kuuliza maswali kadhaa. Wanajeshi wa JWTZ walimjibu kwa uangalifu mkubwa. Majibu hayo, na jinsi yalivyotolewa, yalimridhisha rubani huyo. Kwa hiyo akaachana na uamuzi wake wa kwenda kutua Entebbe, akabadilisha mwelekeo akarudi kutua Mwanza.

Mara tu baada ya ndege hiyo kutua kwenye uwanja wa Mwanza ikawa tayari imezingirwa na wanajeshi wa JWTZ ambao, hata hivyo, walishangazwa sana kuona kuwa badala ya kuwa ni ndege ya Libya na yenye silaha, wakakuta ni ndege ya mizigo ya Shirika la Ndege la Ubelgiji, Sabena, iliyokuwa safarini kwenda kubeba kahawa kutoka Uwanja wa Ndege wa Entebbe kupeleka Djibout.

Hakukuwa na namna ya kuiachia ndege hiyo iondoke Mwanza iendelee na safari zake kwa sababu vifaa vya kuisaidia ndege hiyo, Boeing 707, kuondoka uwanjani hapi havikuwapo uwanja wa ndege wa Mwanza.

Nyerere alipigiwa simu kuombwa ushauri. Aliagiza wafanyakazi wa ndege hiyo wapelekwe Mwanza Hoteli na wapewe vyumba na mlo mzuri kadiri ilivyowezekana. Kisha Nyerere akamwita balozi wa Ugelgiji na kumwambia kilichofanyika nin bahati mbaya na hakukuwa na lengo baya.

Kesho yake ndege ya kijeshi ilipeleka vifaa vya ndege hiyo kutoka Dar es Salaam. Sabena iliwashwa na kuendelea na safari zake.

Itaendelea kesho



Columnist: mwananchi.co.tz