Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Tutumie 2020 – 2025 kujenga mifumo imara (2)

Mon, 24 Sep 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Jumapili iliyopita nilianzisha mjadala kuhusu jinsi ya kujenga mifumo imara ili mazuri yanayofanywa na Serikali yaendelezwe. Leo nahitimisha hoja hii na kufungua mjadala juu ya dhana hii.

Katika sehemu ya kwanza ya mjadala huu nilieleza namna uongozi wa awamu ya tano ulivyoweza kujipambanua na kutumia fedha za walipa kodi kusimamia miradi mikubwa ya maendeleo ambayo italeta mchango mkubwa katika ustawi wa taifa letu.

Nikazungumzia namna uongozi wa Rais John Magufuli ulivyoweza kusimamia masuala sugu na kuifanya nchi inyooke, hayo ni yale ambayo kwa miongo kadhaa tuliyapigia kelele; rushwa na ufisadi, ufujaji wa fedha za umma, nidhamu mbovu za watumishi wa umma, utendaji usio na uwajibikaji kwa watumishi wa umma, ubabe wa wenye fedha dhidi ya wananchi wanyonge na mengine mengi.

Nahitimisha hoja yangu leo kwa kuonyesha mwelekeo wa nchi yetu kuanzia mwaka 2020 – 2025 ambapo tunapaswa kuyatengenezea mkondo wa kudumu.

Mjadala wa yai na kuku

Mara zote, huwa nikitamka maneno “tujenge mifumo imara” watu wengi huhoji ikiwa mifumo imara inajijenga yenyewe au inajengwa na watu. Ukweli ni kwamba watu ndiyo hujenga mifumo, lakini mifumo imara hujengwa na watu imara, viongozi imara au viongozi wanaothubutu.

Kila nchi duniani, ilipofanikiwa kujenga mfumo fulani imara lazima walikuwako viongozi au kiongozi imara aliyeongoza ujenzi wa mifumo hiyo. Mfano; umoja, mshikamano na udugu walio nao Watanzania ni suala la kimfumo, si jambo la muda mfupi na halikushushwa tu.

Suala hili la kimfumo halikujileta lenyewe, lilijengwa kwa juhudi za viongozi imara waliowahi kuongoza taifa hili, wakiongozwa na Mwalimu Nyerere.

Afrika Kusini na Marekani

Nchini Afrika Kusini, baada ya mateso ya miongo mingi waliyopata Waafrika weusi kutoka kwa makaburu wa kizungu, isingelitegemewa taifa hilo likaendelea na maisha ya kawaida bila vita baina ya wazungu na watu weusi.

Suala la ustawi na uhusiano mzuri wa wazungu wa Afrika Kusini (makaburu) na weusi walio wengi (wenyeji) halikuja hivihivi, lilitokana na uthubutu na uimara wa viongozi wa ANC na Afrika Kusini, wakiongozwa na Nelson Mandela. Leo, maridhiano ya wazungu na weusi nchini Afrika Kusini yanaonekana yamo kwenye mfumo lakini hayakuanza tu yenyewe, yalijengwa na viongozi imara.

Pale Marekani, muungano wa mataifa mengi umeweza kujenga taifa moja imara, utumwa ukakomeshwa, serikali ya muungano ikaimarishwa hadi leo na uchumi wa nchi hiyo ukafanywa kuwa wa kisasa zaidi duniani. Mambo yote haya ambayo leo wanadamu wanayatazama kama mfano wa kuigwa ni mambo yaliyojengwa kimfumo, hayakushuka kama mvua kutoka mawinguni. Yalijengwa kwa juhudi kubwa, uimara na uthubutu wa viongozi imara na wenye kuthubutu wa wakati huo, wakiongozwa na Abraham Lincoln, rais wa 16 wa Marekani kati ya Machi 1861 hadi alipouawa Aprili 1865.

Watu imara hujenga mifumo imara

Ni wazi kuwa, na kwa kuzingatia mifano hiyo hapo juu, mifumo imara haijizai, hujengwa na watu, hujengwa na viongozi imara, wenye kuthubutu na maono, hujengwa na viongozi ambao wanayatazama mataifa yao kwa miaka 500 ijayo, vizazi na vizazi vya kesho kuliko leo. Ikiwa nchi yenu inabahatika kupata kiongozi ambaye mnakubaliana hadharani au sirini kuwa ni kiongozi imara, asiyeyumba, mwenye dira na maono – huo ni wakati mzuri wa kumsukuma na hata kusaidiana naye kujenga mifumo imara ndani ya nchi yenu.

Tanzania inaweza kutumia juhudi za sasa za Rais Magufuli, kuzichambua na kuchukua maeneo imara, ambayo ni mengi na kuyatumia kama mifano chanya ya kuiingiza kwenye kitabu cha kudumu cha mfumo wa uendeshaji wa nchi yetu.

Mbinu zinazotumiwa na uongozi wa awamu hii katika ubunifu, utekelezaji na usimamiaji wa miradi mikubwa ya maendeleo, zingelitumiwa na kila awamu tangu Ali Hassan Mwinyi, Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete, leo hii tungelikuwa mbali sana.

Leo hii tusingelikuwa tunajenga reli wala kufufua shirika la ndege, maana hiyo kazi ingelifanywa wakati wa Mwinyi au Mkapa, leo hii tusingelikuwa tunatafuta umeme wa uhakika katika nchi yetu maana kazi hiyo ingelifanywa na awamu ya Mkapa au Kikwete.

Mchango wa marais wastaafu

Simaanishi kwamba Mwinyi, Mkapa na Kikwete hawakuwa viongozi imara, la hasha. Namaanisha kuwa, kama viongozi wa awamu hizo wangelitumika vizuri nyakati zao, masuala makubwa yakaibuliwa na kusimamiwa na kwamba utaratibu huo wa kuibua masuala hayo, kuyatekeleza na kuyasimamia ungelikuwa ni utaratibu wa kimfumo, leo tungelikuwa tunaulizana namna bora ya kufanya uwekezaji kuliko kutafuta umeme wa kudumu.

Kama hatukuwatumia watu imara kujenga mifumo imara wakati wa Mwinyi, Mkapa na Kikwete, hatuna budi kufanya hivyo hivi sasa ambapo hatupingani kwenye hoja kuwa nchi yetu inahitaji kujenga mifumo imara.

Kwa sababu tunakubaliana kuwa mifumo imara haishuki kutoka mbinguni, kwamba inajengwa na viongozi wenye maono, uthubutu na uimara, basi jambo hilo tunapaswa kulifanya hivi sasa, wakati ambapo nchi inaye kiongozi anayethubutu na mwenye uimara wa kutenda lolote lile ilimradi kiu yake ya kuona taifa lenye maendeleo inafikiwa.

Mifano dhahiri

Kwa mfano, mtindo wa utendaji wa sasa wa Serikali ambapo urasimu umepunguzwa, siyo jambo linalopaswa kuishia na uongozi wa JPM, linapaswa kuwa la kudumu, lizamishwe kwenye mfumo wa utendaji wa Serikali na kusiwepo na mkuu yeyote wa nchi ambaye atakuja kulivunja baada ya JPM, sanasana kila kiongozi ajaye baada ya JPM awe na kazi ya kukazia hapohapo au kuongeza utendaji wa Serikali isiyo na urasimu kupita kiasi.

Kwa mfano, mtindo wa sasa wa uibuaji, utekelezaji na usimamizi wa miradi mikubwa ya maendeleo ambayo baadaye hugeuka kuwa kichocheo kikubwa cha maendeleo kama ujenzi wa reli ya kisasa, ufufuaji ATCL, Mradi wa Umeme wa Stiegler na Ujenzi wa Bomba la Mafuta Uganda hadi Tanga – vinapaswa kuwa masuala ya kudumu. Yaani, utawala wa sasa wa JPM ubuni miradi mingine mikubwa na kuiwekea misingi ya utekelezaji ndani ya miaka mitano ijayo, kumi, ishirini, thelathini na zaidi ya hapo.

Mifumo imara na maono ya mbele

Maono ya sasa ya mahitaji ya taifa lenye maendeleo yaanze kujengewa misingi isiyofutika, akiondoka JPM madarakani, Rais ajaye na uongozi wake ajue ya kwamba yako masuala makubwa yanayopaswa kusimamiwa na utawala wake na kwamba masuala hayo ndiyo ajenda za kitaifa na vipaumbele vya maendeleo ya viongozi na uongozi wowote ujao.

Rais ajaye atakuwa na chaguo pia la kuanzisha masuala yake, lakini kwa vyovyote vile hataweza kutikisa ile miradi mikubwa ambayo ni vipaumbele vya taifa kwa wakati aliokabidhiwa nchi. Kwa mfano, tukiwa na mfumo imara itatusaidia ndani ya muda mfupi ujao tuwe na Reli nyingine za kisasa kutoka Kagera hadi Mara, Mara hadi Arusha, Arusha hadi Tanga, Tanga hadi Dar es Salaam, Dar res Salaam hadi Mtwara, Mtwara hadi Ruvuma hadi Mbeya, Mbeya hadi Iringa hadi Kagera.

Naam, kama leo tunaweza kujenga reli ya kisasa kutoka Dar hadi Mwanza na huenda Tabora hadi Kigoma, kwa nini awamu ijayo isiwe na malengo ya kutujengea reli nyingine ya kisasa kutoka mikoa kadhaa kwenda mikoa mingine? Lazima tuwe na mikakati endelevu katika taifa, lakini hatutaweza kujenga mikakati hiyo na kuitekeleza ikiwa hatutatumia faida ya kuwa na kiongozi imara kujenga mifumo imara wakati wake.

Shughuli endelevu

Suala la ujenzi wa mifumo imara siyo kazi ya utawala mmoja, walau mtawala mmoja na awamu yake hujenga msingi imara kwa baadhi ya masuala kama anavyofanya JPM kwenye maendeleo, mapambano dhidi ya rushwa, mapambano dhidi ya dawa za kulevya, matumizi mbaya ya fedha za umma na mambo kama hayo.

Utawala wa JPM ukiondoka, ukija utawala ambao hautakuwa umejengewa mipaka, tusishangae Tanzania ikarudi enzi za rushwa na ufisadi mkubwa, enzi za kusimamia miradi ya maendeleo ya kugusagusa, enzi za urasimu mkubwa kwenye sekta za umma na mengineyo.

Kwa kadri tunavyokosa muunganiko kati ya kiongozi imara, mifumo imara na uongozi unaofuatia baada yake ndivyo ambavyo tunazidi kuchanganyikiwa katika kuifanyia kazi dhana ya ujenzi wa mifumo imara.

Kwa kadri tutakavyoweza kujenga muunganiko kati ya viongozi imara tulionao kama JPM kwa kuwekeza matokeo ya uthubutu wao wa maendeleo kwenye mifumo yetu na kuiwekea kingo mifumo hiyo wakati tunakabidhi madaraka kwa viongozi wanaofuatia, ndivyo tutakavyoweza kutegua kitendawili cha ujenzi wa mifumo imara.

Ndiyo maana nikasema, kipindi cha 2020 – 2025 tuwekeze kwenye ujenzi wa mifumo imara. Mada hii inaweza kuwa ngumu sana, lakini hatukwepi kuijadili. Nilichofanya ni kuihitimisha kwa kufungua mjadala zaidi.

Julius Mtatiro ni mtafiti na mchambuzi wa utendaji wa Serikali barani Afrika; ni mwanasheria, mfasiri na mtaalamu mshauri wa miradi, mtawala na mera. Barua Pepe; [email protected])

Columnist: mwananchi.co.tz