Kabla ya dunia kufika mwisho vitatokea vitu vingi sana, lakini kamwe haitatokea mwanaume kushinda mabishano ya kihisia dhidi ya mwanamke; yaani yale mabishano ya kitoto yanayofanywa na watu wazima usitegemee kushinda ‘anko’, labda zitumike njia nyinginezo nje ya mazungumzo.
Kwa kuongea tu wanawake wanatuzidi kila kitu kasi ya kuchakata maneno, idadi ya misamiati, pumzi za kuzungumza na mbinu za kumshinda mtu, huenda taaluma hii inaishi ndani ya damu zao, wamezaliwa nayo.
Kwa sababu hatuwezi kuwazidi, basi angalau tufahamu mbinu chache wanazotumia.
Unaingia chumbani, mwanamke anachezea simu yake, unamsemesha hakujibu, yuko ‘bize’ na simu. Unaamua kutumia uanaume kidogo, unafoka ili kuonyesha unachukizwa na anachokifanya. Anashtuka, unamuuliza; ‘unaangalia nini kinachokufanya uwe bize mpaka hunisikii?’
Ukishamuuliza swali la hivi, mwanamke anachokifanya ni kukulisha maneno, yaani anakunukuu kwa maneno ambayo hukuyatamka; ‘Kwa hiyo nisitumie simu siku hizi?’ anakuuliza, akimaanisha hicho ndicho alichosikia ukizungumza.
Pia Soma
- Mgombea urais wa Tunisia ajitoa kwenye kampeni za uchaguzi
- Tiwa Savage: Wizkid hajanitongoza, sina uhusiano naye
- Tembo sita wafa maji wakijaribu kumuokoa kichanga Thailand
- Watu 100 wafariki maandamano ya Iraq
Ili kumkosoa, unajitetea kwamba ‘sikukwambia usitumie simu, nimekuuliza ulikuwa unawasiliana na nani?’
Atakachokifanya baada ya hapo ni kukusingizia, atakwambia ‘Unataka nisiwe nazungumza na watu kwa simu? Au unadhani kila mtu ni kama wewe, akiwa anatumia simu basi anafanya mambo ya ajabu ya kuchati na watu wa ajabu ajabu? Na tangu umekuja hapa nimekuona una mahasira yako, unanitafutia sababu tu, au unadhani mimi sikujui ukiwa na mahasira yako ulikotoka nayo huko nje, au unaona hiyo mijanamke yako unayochatigi nayo kwenye simu ndo inakujua zaidi ya mimi.’
Kwa sababu unajua hutomshinda, unaamua kumaliza ugomvi, unamwambia ‘Basi yaishe, tusije kugombana kwa sababu za kijinga.’
‘Ahaa! Kwa hiyo mimi mjinga na naongea ujinga?’ atakuuliza.
Hapo utakuwa tayari umeshasingiziwa mambo matatu. Kwanza unatumia simu yako kufanya ushenzi na mambo ya ajabu ajabu. Pili una wanawake tofauti na yeye na isitoshe ni kwamba unadhani wanakujua kuliko yeye anavyokujua. Na tatu ni umesema yeye ni mjinga.
Hatua inayofuata sasa ni kuongeza timu yake, hapa anachokifanya ni kuhakikisha kuwa haya mabishano hayawi kati yako na yeye tu, bali kati yake na watu wengine wengi waliopo upande wake.
Atakwambia ‘Na nyoka hutoka kwa nyoka, kwa hiyo mimi mjinga, baba yangu mjinga, mama yangu mjinga na familia yangu yote wajinga si ndio?’
Hapo tayari ameshaongeza wanachama wake, timu yake imekuwa kubwa, na sasa hushindani na yeye pekee, bali familia yake nzima na usipokuwa makini, mkishafikia hatua hii, tatizo linaweza kuwa kubwa kweli na kutoka nje ya chumba chenu na kuwafikia hadi wakwe.
Si lazima kila ugomvi ufuate mtiririko huu, lakini haya yote manne yana nafasi kubwa ya kutokea na ndo yanayosababisha tushindwe kwenye mabishano nao.