Kabla hatujafika mbali naomba turudie kusoma kichwa cha habari. Kimeandikwa ‘Pesa zinatupa wanawake wepesi’ hakisemi ni dhambi kuwa na pesa au kutafuta pesa.
Pesa ni nguvu, na nguvu ni kitu muhimu kuliko kitu chochote hapa duniani. Hata kabla ya kuanza mfumo wa pesa za karatasi tunazotumia leo, pesa zilikuwa zinatumika.
Binadamu wa kale alitumia nguvu na maarifa kama pesa, ili apate chakula ilibidi atumie vitu hivyo viwili kuwinda sungura au kupanda juu ya mti kuangusha fenesi kwa wakati ule hiyo ndiyo ilikuwa pesa.
Ukiweka pembeni kazi za Mungu tu, pesa inaweza kufanya kila kitu kingine kinachobaki chini ya jua kununua muda, kununua akili, kununua afya bora, kununua heshima, kununua pesa zingine yaani inaweza kufanya kila kitu.
Ukiwa na fedha utakuwa na marafiki wengi, utapendwa na kila mtu, utaheshimiwa na utathaminiwa. Lakini changamoto inakuja ni kwamba, ukiwa na fedha kuna baadhi ya mambo huwezi kuyapata kiuhalisia. Kwa mfano, kupata mwanamke ambaye unatamani ni vigumu.
Kwa nini? Kwa sababu fedha ina kawaida ya kutojificha, ukiwa na fedha lazima watu watafahamu kwa jicho la kwanza watakaloelekeza kwako. Hata ukijiweka katikati ya kundi kubwa la watu, fedha itakuchomoza juu na kusema nipo hapa, kwa huyu bwana.
Pia Soma
- ANTI BETTIE: Hivi ni dhambi kumuoa mtoto wa mama yangu mkubwa?
- USHAURI WA DAKTARI: Sababu mwanamke kulewa haraka kuliko mwanaume...
- TUONGEE KIUME: Mahari ni mabaki ya utumwa yaliyopewa jina zuri
Na hii ndiyo sababu tunasema fedha zinatupa wanawake wepesi.
Mwanamke imara na mzuri ni yule ambaye anahitaji pesa sana sana, lakini hayuko tayari kufanya kinyume na matakwa yake au kufanya vitu visiyompendeza ikiwemo kuwa na mtu ambaye hampendi ili tu apate hizo pesa anazozihitaji sana.
Mwanamuziki wa Tanzania, Wakazi aliwahi kuandika. ‘Mwanamke mzuri ni mwenye tabia njema na mapenzi ya dhati, na mapenzi hayanunuliki kwa fedha. Unaweza kununua tendo la kufanya mapenzi, lakini si upendo’ huu ndiyo ukweli.
Na hii si kwamba tunawalaumu wanawake kwamba wanapenda pesa, hapana. Ukweli ni kwamba tunaongelea wanawake kwa sababu hii kolamu ni Tuongee Kiume, lakini hata wanawake wenye fedha pia, fedha zao zinawapa wanaume dhaifu.
Wanaume walioshindwa kutafuta vyao, wanaotegemea kuhudumiwa.
Mambo mawili muhimu ya kumalizia; kwanza si vibaya kuwa na mweza mwenye fedha, lakini cha kujiuliza ni je uko hapo kwa sababu ya fedha zake, au una sababu iliyo mbali sana na hiyo nguvu yake kiuchumi.
Na pili ni tusiokuwa na hela angalau ya nusu ya tunazozitaka, tuendelee kutafuata kwa jasho na akili.