Ugonjwa huu hushambulia sehemu za uzazi za mahindi. Mashambulizi hufanywa na aina mbili za vimelea jamii ya uyoga (ukungu) vijulikanavyo kwa majina ya kitaalamu kama Sphacelotheca reliana na Ustilago maydis. Vimelea hivyo husababisha magonjwa ya aina mbili ambayo dalili zake zinafanana.
Mimea iliyoshambuliwa na ugonjwa huu ama haizai kabisa ama inazaa kiasi kidogo ukilinganisha na jinsi ambavyo ingeweza kuzaa kama isingekuwa imeshambuliwa.
Dalili zake huwa kuota kwa uvimbe katika sehemu za mmea zinazokua kama vile punje
za mahindi, mbelewele na hata kwenye majani. Uvimbe huo ukikauka na kupasuka hutoa vumbi jeusi kama masizi ambayo ndiyo viini vya/mbegu ya huo ugonjwa.
Dalili ya msingi ya ugonjwa huu kwenye mhindi ni kwamba inawezekana kuwa na baadhi ya punje zilizoshambuliwa na zingine ambazo hazina dalili katika gunzi moja.
Udhibiti wa ugonjwa huu
Moja, tumia mbegu bora ingawa mpaka sasa haipo mbegu maalumu yenye kustahimili ugonjwa huu. Kwa kutumia mbegu bora, mkulima utajihakikishia mavuno bora.
mbili, daima hakikisha unalima kilimo cha kisasa kikijumuisha urutubishaji wa udongo. Epuka kuijeruhi mimea uwapo shambani. Mimea iliyo na majeraha hushambuliwa kwa urahisi na ugonjwa huu. Pia dhibiti wadudu waharibifu ambao pamoja na madhara mengine wanayosababisha pia huijeruhi mimea na kwa hivyo kurahisisha maambukizo ya ugonjwa huu.
Tatu, kila inapowezekana tumia kilimo cha kubadilisha mazao.
Nne, unapolima hakikisha masalia mabua yamefukiwa chini sana.