Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Serikali inafanyia kazi kero ya mafuriko?

18089 Pic+mafuriko TanzaniaWeb

Wed, 19 Sep 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Wiki iliyopita Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini (TMA) ilitangaza msimu wa mvua za vuli zinazotarajiwa kuanza Septemba hadi Oktoba mwaka huu.

Kwa mjibu wa Mkurugenzi wa TMA, Dk Agnes Kijazi, mvua hizo zinatarajiwa kuwa za wastani hadi juu ya wastani kwa maeneo mengi nchini.

Ongezeko la mvua hizo linatarajiwa katika mwezi Novemba na kuna uwezekano wa kutokea vimbunga katika eneo la kusini magharibi mwa Bahari ya Hindi.

Zipo athari zinazoweza kutokea ikiwemo hali ya unyevunyevu wa udongo katika maeneo mengi yanayotarajiwa kuwa na mvua za wastani na juu ya wastani na kwamba shughuli za kawaida za kilimo katika maeneo mbalimbali nchini zitaathiriwa.

Katika kipindi hicho vipindi vifupi vya mvua kubwa vinatarajiwa kujitokeza na hivyo kuongeza uwezekano wa mafuriko hata katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za wastani hadi chini ya wastani.

Wakati utabiri huo unatolewa, Watanzania bado tuna kumbukumbu ya matukio ya mafuriko yaliyotokea katika msimu wa mvua zilizonyesha mwanzoni mwa mwaka huu ambazo zilisababisha mamia ya wakazi katika maeneo mbalimbali nchini kuathirika.

Miongoni mwa mikoa iliyokumbwa na mafuriko hayo ni pamoja na Dar es Salaam, Morogoro na Mwanza kwa uchache huku wakazi waliokuwa wanaishi mabondeni nyumba zao ziliingiliwa maji na hivyo kukosa sehemu za kuishi.

Nikitolea mifano jijini Mwanza watoto wawili wa familia moja walifariki dunia na wengine watatu kujeruhiwa baada ya kuangukiwa na nyumba waliyokuwa wanaishi kutokana na mvua zilizokuwa zinanyesha jijini humo.

Matukio mengine ya namna hiyo yalitokea wilayani Kwimba ambako kwa mujibu wa aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Kwimba, Mtemi Msafiri watu 13 walijeruhiwa na nyumba 479 zikiwemo vyumba viwili vya shule ya msingi Mangulumwa na maabara ya sekondari Igongwa ziliezuliwa na upepo kufuatia mvua kubwa iliyonyesha.

Wakati tukijipanga kwa msimu mwingine wa wa mvua tunapaswa kujiuliza, je, Serikali na wananchi wamefanyia kazi kwa kiwango gani changamoto hizo, ili kuhakikisha madhara na matukio kama hayo hayajitokezi?

Pamoja na changamoto ya watu kujenga na kuziba mifereji ya kupitishia maji, Serikali imechukua hatua gani kuhakikisha wanaoishi mabondeni wanatengenezewa mazingira salama ya kuishi ili kuwaepusha na athari kama hizo?

Ukiachilia mbali suala la watu kujenga kwenye mifereji lakini pia lipo tatizo la uharibifu wa mazingira ambalo kwa muda mrefu Serikali imekuwa ikilipigia kelele na kuwahamasisha wananchi kupanda miti kuzuia uharibifu wa mazingira, lakini hakuna mrejesho kuhusu kiasi gani wamefanikiwa?

Huenda jibu likawa ndiyo kwa baadhi ya maeneo, hasa pale ambapo wamepanda miti ya kutosha kuzuia uharibifu wa mazingira hususani maeneo ya mjini lakini kwa vijijini ambako kuna waathirika zaidi suala hilo limefanikiwa kwa kiwango gani?

Kutokana na utabiri huu kunahitajika jitihada za ziada kuwaelimisha wananchi kuelewa madhara ya ukataji miti ovyo kwa ajili ya kuni na mkaa ili kupunguza changamoto hizo.

Rai yangu ni kwamba kila mmoja kwa utashi wake asaidie kutatua changamoto za uharibifu wa mazingira ili kuepusha madhara kama hayo yaliyotukumba katika msimu uliopita.

Columnist: mwananchi.co.tz