Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) lilifunga kalenda ya nusu karne Ijumaa ya Mei 30, mwaka huu kwa masimulizi na ushuhuda wa safari ndefu kutoka kwa Mwenyekiti wake wa Kwanza, Silyvesta Barongo aliyeonyesha matumaini ya kwanza ya ugunduzi wa gesi asilia mwaka 1974 katika kisiwa cha Songosongo.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Angellah Kairuki aliyemwakilisha Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alitumia fursa hiyo kusisitiza uwekezaji zaidi katika shughuli za utafiti kwa miaka ijayo, akisema bila tafiti shirika hilo lisingeweza kujivunia mafanikio yaliyopatikana ndani ya miaka 50.
Kwa mujibu wa TPDC, shughuli za utafutaji mafuta na gesi asilia nchini zilianza takribani miaka 60 iliyopita. Mwaka 1952 Kampuni ya Petroli ya Uingereza (BP) na Kampuni ya Shell ya Uholanzi zilianza utafutaji wa mafuta katika maeneo yote ya pwani ya Tanzania.
Kaimu Meneja Mtafiti kutoka Idara ya Mkondo wa Juu wa Shirika hilo, Shigela Josephat anasema tangu kipindi hicho hadi sasa, jumla ya visima virefu 96 vimechimbwa vikijumuisha vya utafutaji, uendelezaji na uzalishaji.
Anasema hadi sasa Taifa lina vitalu zaidi ya 20 vilivyo wazi kwa ajili ya uwekezaji mpya kwa maeneo ya nchi kavu na baharini huku leseni 11 zikiendelea kufanya kazi chini ya umiliki wa TPDC.
Kwa mujibu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA), kampuni zinazofanya shughuli za utafiti, uendelezaji na uzalishaji kupitia leseni hizo ni Kampuni ya Mafuta ya Shell Tanzania, Pan African Energy Tanzania (PAET), Heritage Oil, Ndovu Resources Ltd, Equinor na Swala.
Pia Soma
- Pongezi ya Nape kwa Waziri Makamba yaibua mjadala
- Watu 14 wauawa kwa bomu Syria
- Jeshi latawanya waandamaji Sudan, wawili wauawa
- Wabunge waridhia kukatwa posho kumchangia mama wa pacha wanne