Nina mpenzi ana fedha za kutosha kutokana na miradi anayofanya na kazi nzuri ya kumuingizia kipato cha kutosha. Tatizo hanipi fedha, akinipa sana tena nimejituma Sh100,000 tu.
Naomba mbinu za kumbana anipe fedha za kutosha.
Nifanyeje?
Mirianne
Moshi
Hakuna mbinu za kumbana ili mwenzi wako akupe fedha zaidi ya kauli njema wakati wa kuomba na ufafanuzi wa kina unataka kuzifanyia nini. Hali ni ngumu hakuna anayetoa fedha za kuchezea zaidi ya kufanyia mambo ya msingi, hivyo ukitaka akupe nyingi kuwa mbunifu naamini hawezi kukataa kukupa fedha za maendeleo, lakini ukiomba za mawigi, kusuka, kwenda ngomani kwa shoga, utaendelea kupata hizo hizo hata ukijituma kupindukia.
Anti pole na kazi, kuna kijana nampenda ni mzuri, akivaa anapendeza na ni mpole, lakini aina ya mapenzi yake unaviondoa vyote hivi katika akili yangu. Nilijaribu kuishi naye baada ya kutoa posa kwetu nikidhani nitambadilisha huu ni mwezi wa sita nimeshindwa. Bwana huyu akipanda punda saa nne hashuki hadi saa saba au nane tena kwa shingo upande.
Nifanyeje?
Somoe
Mtama
Pole Somoe ndiyo ukubwa huo. Nakushauri mwambie kwanza kabla ya kufanya maamuzi yoyote kuwa anakuchosha kutokana na aina ya mapenzi yake. Kama unapata maumivu ambayo yanadumu muda mrefu kutokana na aina ya mapenzi anayokupa zungumza na daktari uende naye akamueleze madhara ya kiafya unayoweza kuyapata kutokana na jambo hilo kukithiri.
Usikubali kuolewa naye kabla hujaliweka sawa hili, itakupa shida na utakuwa mtumwa.
Nina umri wa miaka 36. Nimechoka kutoka na waume za watu au wapenzi ambao baadae ninanyang’anywa kwa sababu sina haki miliki nao.
Nifanyeje?
Nahisi unakurupuka kupenda madhara yake unaangukia kwa waume za watu hilo ni kosa jipange upya. Nakushauri tulia katika wengi wanaokutaka au kukutamani kimapenzi katika vigezo vyako ulivyonavyo, katika kupenda hakikisha kuwa hana mke kiwe kikuu labda tu atakapokuja mwenye mke Muislamu anayeonyesha nia ya kukuoa mke wa pili au wa tatu kwa sababu kwao imehalalishwa, lakini kwa wengine kuwa makini. Kumpata wako si kigezo cha kutonyang’ anywa ila itakupa uhalali wa kuhoji hilo likitokea, hili ni angalizo kwako. Tulia utampata wako ukilazimisha utaokota magarasa ambayo yataendelea kukusumbua na umri si kigezo cha kukimbilia kuolewa.