Dar es Salaam. Katika kukabiliana na changamoto ya masoko katika kilimo, wakulima nchini Tanzania wametakiwa kubadilisha mbinu ya kulifikia soko.
Rai hiyo imetolewa leo jioni Alhamisi Mei 23, 2019 na mwandishi wa vitabu, Charles Nduku katika mjadala wa Jukwaa la Fikra ulioandaliwa na kampuni ya Mwananchi Communications Ltd( MCL) na kurushwa moja kwa moja na kituo cha Televisheni cha ITV na Redio One.
Nduku amesema wakulima wana wajibu wa kufanya utafiti hasa wa soko kulingana na wanachotaka kulima.
“Mkulima afike sokoni kwanza aulize ni kitu gani mlaji anahitaji, ni bidhaa yenye ubora upi soko linahitaji, ni kwa ukubwa upi soko linahitaji bidhaa yako.”
"Ni kwa namna gani itafika sokoni, wakati gani uhitaji unakuwa juu, na vitu gani vya kuzingatia kabla bidhaa haijafika sokoni,” amesema Nduku.
Katika maelezo yake amefafanua kwamba mbinu hizo zitasaidia kuondoa changamoto za kuzalisha na kukosa soko, lakini pia itasaidia kumwongoza mkulima kulima, katika mazingira gani ya uzalishaji.
Pia Soma
- Mkulima wa vitunguu Iringa aiangukia Serikali
- Mkulima: Vijana geukieni kilimo hiki msisubiri kuajiriwa
- MWANANCHI JUKWAA LA FIKRA: Mkombozi wa mkulima fedha za mikopo ya benki ni vikundi
"Tunahitaji kutumia hii mbinu itapunguza presha ya soko na kupeleka bidhaa na wakati sahihi sokoni. Mkulima lazima aanzie kwa mteja kabla ya kuzalisha chochote,” amesema Nduku.