Dodoma. Serikali ya Tanzania imesema ulipaji kodi kwa hiari umesaidia mapato yake kupatikana kwa kiasi kikubwa.
Hayo yameelezwa bungeni mjini Dodoma leo Jumatano Januari 29, 2020 na naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Ashatu Kijaji katika mjadala wa taarifa za kamati ya Bunge za Hesabu za Serikali (PAC) na Hesabu za Serikali za Mitaa (Laac).
Dk Kijaji amesema Watanzania kulipa kodi haina mjadala na ndio jambo linalotakiwa ili nchi isonge mbele.
Amesema mwaka 2019 katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2019 Serikali ililenga kukusanya Sh9.45 trilioni lakini ikakusanya Sh9.1 trilioni sawa na asilimia 96.3 ya malengo.
"Jambo hilo ni jema lakini Watanzania lazima walipe kodi tena iliyostahiki, tunaona huo ni mpango mzuri wa maendeleo na bila shaka tutafika," amesema Dk Kijaji.