Dar es Salaam. Huenda mwanamuziki Harmonize hakutoa mwaliko kwa baadhi ya wasanii na wadau wa muziki wa Bongo Fleva kuhusu kufunga ndoa na Sarah Michelotti.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumapili Septemba 8, 2019, Said Fella mmoja wa mameneja wa msanii Naseeb Abdul maarufu Diamond amesema hakuwa na taarifa kuhusu kufungwa kwa ndoa hiyo.
Jana Jumamosi Septemba 7, 2019, Harmonize alifunga ndoa na Sarah, raia wa Italia ikiwa ni mwezi mmoja tangu alipomvalisha pete ya uchumba nchini Italia.
Ndoa hiyo ya Kiislamu ilifuatiwa na sherehe iliyohudhuriwa na watu 100 na kufanyika katika Hoteli ya Serena, jijini Dar es Salaam.
"Licha ya kuwa nipo Iringa naandaa tamasha la Wasafi sikuwa na taarifa kama Harmonize anaoa,” amesema Fella akibainisha kuwa alianza kufahamu jambo hilo baada ya kuona picha mitandaoni.
"Ilikuwa siri maandalizi yalifanywa kwa siri na wenyewe walitaka iwe hivyo, nadhani walitaka kufanya jambo la kushtukiza,” anaeleza mmoja wa marafiki wa mwanamuziki huyo kwa sharti la kutotajwa jina.