Lifestyle

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

SIL

Archraf Hakimi awakumbuka wenye uhitaji Tanzania

Hakimi Archraf Hakimi awakumbuka wenye uhitaji Tanzania

Fri, 28 Jun 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Mchezaji wa kimataifa wa soka kutoka Morocco anayechezea timu ya PSG, Archraf Hakimi juzi ametoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa wanafunzi zaidi ya 400 wenye uhitaji maalum kwenye shule ya Sekondari ya Patandi ya jijini Arusha vyenye gharama ya zaidi ya bilioni moja.

Baadhi ya vifaa hivyo ni pamoja na komputa zaidi ya 50, samani, vifaa maalum alama nundu, Mashine za kuchomea taka na kuchemshia maji.

Katika hafla hiyo ambayo Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Angellah Kairuki alikuwa mgeni rasmi ambapo aliwakilishwa na Katibu Mkuu wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi mchezaji huyo ameipongeza Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa jitihada kubwa zinazofanyika katika kutoa huduma za elimu kwa watoto wenye uhitaji maalum.

Mchezaji huyo ambaye ni mara yake ya kwanza kutoa misaada kupitia taasisi yake nje ya nchi ya Morocco ameuhakikishia Serikali kuwa ataendelea kushiriki kikamilifu kutoa misaada kwa jamii hapa nchini.

Aidha, Hakimi ambaye ameletwa nchini kwa mwaliko maalum wa Rais wa Yanga Mhandisi Hersi Said amesema amevutiwa na vivutio vya Utalii na kuahidi kuja tena.

Hakimi ni miongoni mwa wachezaji nguli duniani ambaye anawafuasi zaidi ya milioni 20 duniani pia ameshukuru Yanga, Wizara ya Maliasili na Utalii na Bodi ya Utalii kwa uratibu mzuri wa ziara yake.

Kwa upande wake Dkt. Abbasi amemshukuru Hakimi kwa misaada yake na Mhandisi Hersi kwa kusaidia kuleta watu mashuhuri kama Hakimi ambao wanashaidia kutangaza utalii wa Tanzania na kutoa wito kwa watu wengine kufanya hivyo.

“Nakumbuka siku ambayo Injinia ulikutana na Hakimi Paris ulinipigia simu kuwa una “surprise” na ukasema tunataka kumletea Hakimi nikasema sawa kabisa mlete” amefafanua Dkt. Abbasi.

Aidha, Dkt. Abbasi ameendesha harambee ya kuchangia shule hiyo ambapo Klabu ya Yanga imetoa vitanda 40 na magodoro yake, na wadau wengine ambao waliweza kutoa zaidi ya milioni mbili na laki sita na ahadi ya milioni 3.

Injinia Hersi amempongeza Mkuu wa shule ya Sekondari ya Patandi kwa ufanyaji kazi wake ambapo pia amefafanua kuwa wazo la kuichagua shule ya Sekondari ya Patandi lilitoka kwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe Angellah Kairuki.

Katika hafla hiyo wizara imeweza kumpatia zawadi Hakimi, Rais wa Yanga na Mkuu wa shule ya Sekondari ya Patandi Janeth Mollel kabla ya Hakimi kucheza mpira na vijana wafuasi wa Yanga.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live