Dar es Salaam. Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) linatarajia kuongeza gawiwo kwa serikali kutoka Sh1.5 bilioni kwa mwaka 2017/2018 hadi Sh 2.5 bilioni mwaka ujao wa fedha.
Hayo yamesemwa leo Julai 5 na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Waziri Kindamba wakati wa maonyesho ya kimataifa ya biashara maarufu, Sabasaba mara baada ya kuibuka mshindi katika kundi la kampuni zinazotoa huduma za mawasiliano nchini.
Amesema hii inatokana na hali ya soko inavyoonekana tangu lilipotolewa gawiwo la kwanza.
Amesema shirika hilo ni la kizalendo na kwa mwaka wa fedha ujao 2018/19 wanatarajia kuongeza gawiwo serikalini mara mbili ya walichotoa kwa mwaka wa fedha ulioishia Juni 2018.
"Tunaweza kuongeza gawiwo kutoka Sh1.5 bilioni ya mwaka wa fedha ulioishia Juni 2018 kufikia 2.5 hadi 2.7 kutokana na hali ya soko inavyoonekana, fedha hizi ni za Watanzania ndiyo maana zinaelekezwa hazina kwa ajili ya kusambazwa kwenye huduma za jamii," amesema Kindamba.