Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

VIDEO: Flyover ya Tazara yaanza kutumika, wananchi wanena

Video Archive
Mon, 17 Sep 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Kuanza kutumika kwa barabara ya juu katika makutano ya Barabara za Nyerere na Mandela (Tazara)  kumepokewa kwa hisia tofauti na wananchi.

Wakati wengi wakipongeza, hali imekuwa tofauti kwa wafanyabiashara ndogondogo waliodai kuwa kwa sasa hakutakuwa na foleni hivyo biashara zao hazitauzika.

MCL Digital ilipiga kambi katika daraja hilo leo Septemba 15, 2018 na kuzungumza na watumiaji, huku ikishuhudia magari yakipita na hali imebadilika hapakuwa na foleni.

Aprili 16, 2016 Rais John Magufuli aliweka jiwe la msingi katika barabara hiyo huku Agosti 29, 2018 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akieleza kuwa ujenzi huo ulikuwa umekamilika kwa asilimia 98 na ufunguzi utafanyika Oktoba.

Kondakta wa daladala linalofanya safari zake kati ya  Vigunguti-Temeke, aliyejitambulisha kwa jina moja la Said amesema kukamilika kwa daraja hilo kutasaidia kuongeza idadi ya safari  walizokuwa wakifanya kwa siku, hivyo kujiongezea kipato.

“Foleni ya eneo hili (Tazara) ilituumiza sana sisi watu wa biashara ya usafiri. Tulikuwa tunafanya safari nne za kwenda na kurudi kwa siku lakini kwa sasa tunakwenda safari nyingi zaidi kwa kuwa foleni hakuna,” amesema Said.

Wansislaus Shoo, aliyekuwa na gari binafsi amesema kabla ya kufunguliwa kwa barabara hiyo, alitumia wastani wa saa mbili  kupita eneo hilo jambo lililoathiri shughuli zake za biashara.

Hata hivyo, mfanyabiashara wa mihogo na karanga eneo la Tazara, Neema Chaula amesema kabla ya kuwapo kwa barabara hiyo, alikuwa akipata Sh4,000 hadi Sh4,500 lakini hadi leo saa 8:00 mchana ameuza Sh500 tu.

Awali, ofisa mtendaji mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), Patrick Mfugale amesema kukamilika kwa mradi huo utapunguza muda wa kukaa kwenye foleni kwa asilimia 80, akimaanisha kutoka dakika 45 hadi dakika 10 za kuvuka kwenye makutano hayo.

Chanzo: mwananchi.co.tz